The House of Favourite Newspapers

NDOA YAKE NA DIAMONDI, TANASHA AANIKA KUFURU YAKE! 

DAR ES SALAAM: Mambo yameiva! Ndivyo unavyoweza kusema kufuatia ndoa ya staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ kubakiza siku chache huku bibi harusi mtarajiwa Tanasha Donna ‘Zahara Zaire’ akianika kufuru yake, Ijumaa lina habari kamili.

Kwa mujibu wa maneno yaliyotamkwa na Diamond, ndoa yao inatarajiwa kufanyika Februari 14, mwaka huu siku ambayo ni maalum kwa wapendanao.

 

TAARIFA KWANZA ZA NDUGU

Mitandao mbalimbali ya nchini Kenya ambayo imeeleza kupata taarifa za kufuru za ndoa hiyo kutoka kwa ndugu wa familia ya Tanasha na ndoa hiyo itakuwa ni ya kihistoria kwa mwaka huu 2019 kwani mbali na Diamond kuwa na jina kubwa na ukwasi wa kutosha, ndugu hao wa upande wa mwanamke nao si wepesi kihivyo.

“Tunajua Diamond amejipanga na anajimudu kifedha lakini na sisi huku kama familia hatuko vibaya sana. Tumejipanga vilivyo, wewe vuta picha mtu kama Diamond anafanya kufuru halafu na sisi tuongezee mzigo mezani itakuwaje?” alinukuliwa mmoja wa wanafamilia mtandaoni.

 

MSAFARA USIPIME!

Mwanafamilia huyo alisema wanatarajia kuwa kwenye ndoa hiyo ambayo itakusanya watu wengi mashuhuri, kutakuwa na helkopta maalum ya kubeba maharusi, msafara wa magari kibao ya kifahari.

Alisema mbali na hilo, katika siku nne ambazo wamepanga ndoa hiyo kusherehekewa nchini Kenya, kutakuwa na vyakula, vinywaji vya kufa mtu kwa kila ambaye atakuwa amealikwa.

“Yani siku nne mfululizo watu watakuwa wanakula na kunywa wanachotaka. Kwa wale watakaotaka pombe kali zitakuwepo, vinywaji laini ndio usiseme yani hakuna kupumzika, ni burudani mwanzo mwisho,” alinukuliwa ndugu huyo.

 

WAGENI KUTENGEWA HOTELI

Ndugu hao wa upande wa Tanasha wameeleza kuwa, mbali na vyakula na vinywaji wanatarajia pia kuandaa hoteli maalum ambazo watafikia wageni waalikwa hususan mastaa wa muziki.

“Tunajua Diamond ana marafiki mastaa kutoka Nigeria, Marekani na kwingineko hivyo lazima tuandae hoteli maalum na zenye hadhi ya mastaa,” alinukuliwa mwanafamilia mwingine.

TANASHA ATHIBITISHA

Katika mahojiano ya juzikati ambayo ameyafanya na mtandao maarufu kwa habari za mastaa nchini Kenya, Tanasha aliweka wazi kuwa ndoa yake hiyo itakuwa si ya kitoto kutokana na jinsi ambavyo wawili hao wamejipanga.

Alisema, wanatarajia kuwa ndoa hiyo itakuwa ni ya kipekee kwani itasherehekewa kwa siku nne mfululizo kuanzia siku hiyo ya Valentine ambayo itakuwa Alhamisi, Ijumaa, Jumamosi na Jumapili.

“Tumepanga kuwa sherehe yetu itakuwa ni siku nne mfululizo. Yaani tunafunga tarehe 14 lakini kilele chake kitakuwa tarehe 17 Februari,” alisema Tanasha.

 

FUNGATE DUBAI

Kama hiyo haitoshi imeelezwa kuwa, mara baada ya wawili hao kumaliza sherehe hiyo kwa upande wa Kenya, maharusi wanatarajiwa fungate lao kulifanyia nchini Dubai na watakaporudi watafanya sherehe nyingine Bongo.

 

TUJIKUMBUSHE

Diamond ambaye amezaa na mfanyabiashara maarufu wa Kiganda, Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’, alimwagana na mrembo huyo Februari 14, mwaka jana na baada ya hapo mkali huyo ametajwa kubanjuka na warembo tofauti akiwemo Lilian Kessy ‘Kim Nana’.

Hata hivyo licha ya mama yake mzazi kuonesha kumkubali Kim Nana awe mkwewe, mwishoni mwa mwaka jana, Diamond ‘alichenji’ gia angani na kusema atamuoa Tanasha siku ambayo yeye aliachwa na Zari (Februari 14, mwaka huu).

Stori: ERICK EVARIST, IJUMAA

Comments are closed.