The House of Favourite Newspapers

Njia zinazoweza kumfanya mwanamke asiyezaa azae

MIRIJA ya kupitisha mayai ya mwanamke iliyoziba inaweza kusababisha ugumba, ila bado nafasi ya kupata mimba inakuwapo endapo tu uchunguzi na matibabu sahihi yatafanyika. 

 

Matibabu ya kitaalamu yakifanyika kwa mwanamke mwenye matatizo ya kuziba mirija hiyo ya kupitishia mayai au mbegu, anaweza kushika mimba na kushika mimba kisha kupata mtoto. Kutibiwa na kupata ujauzito itategemeana na ukubwa wa tatizo la mirija kuziba na aina ya matibabu yatakayotumika.Ni rahisi zaidi kutibiwa endapo eneo lililoziba lipo karibu na nyumba ya uzazi.

 

Matatizo yanayosababisha tatizo hili yanaweza kutibiwa na mwathirika kuweza kupata ujauzito baada ya tiba hasa kwa wale wenye kuziba mrija upande mmoja. Njia mbalimbali za kisasa zinaweza kutumika kuzibua mirija hiyo ikiwamo upasuaji ujulikanao kitaalamu kama ‘laparascopic’.

Njia hii inatambulika zaidi kwa sasa kwa kuzibua kirahisi mirija ya kupitishia mayai iliyoziba kiasi. Upasuaji unaweza kufanyika kukarabati mirija hiyo iliyoziba kutokana na madhara ya makovu ya mashambulizi ya bakteria na ya ujauzito uliotunga na kujipachika katika mirija badala ya mji wa mimba.

 

Madaktari wa upasuaji wanaweza kuondoa eneo lenye kovu katika tumbo la uzazi na kuziunganisha pande mbili za mirija zisizo na makovu. Upasuaji huu una matokea mazuri endapo tu makovu yaliyopo katika mirija hiyo yapo kwa wastani.

 

Ingawa dawa za kupevusha mayai mengi inaweza kusaidia kushika ujauzito, hatari ya mimba kutunga na kukua katika mirija huwa ni kubwa na hatimaye upasuaji wa dharura utahitaji kutibu tatizo hili. Vilevile kufanya upasuaji wa dharura kulikabili tatizo la mimba kutunga katika mirija ya mayai nalo linaongeza zaidi hatari ya kujitokeza tena baadaye.

 

Nchi zilizoendelea kitabibu na ujuzi, wanawake wenye tatizo hili hupandikizwa kijiyai kilichorutubishwa na mbegu za kiume katika maabara maalum na njia hii kitaalamu hujilikana kwa jina la ‘In Vitro Fertilization’ (IVF).

Njia hii hupendelewa zaidi na madaktari wa kisasa ili kuepukana na tatizo la mimba kujitunga katika mirija iliyoziba na kuacha upenyo mdogo. Njia hii in­aokoa upasuaji kwani husaidia kupandikiza kiji­yai kilichorutu­bishwa kitaala­mu na mbegu ya kiume moja kwa moja katika nyumba ya uzazi.

 

Ni vigumu kuliepuka tatizo hili la kuziba mirija ya uzazi lakini wanawake wanaweza kupunguza hatari kwa kuepuka ngono na wenza tofautitofauti na utoaji wa mimba usio salama mitaani.  Wasichana wengi hukumbwa na taizo hili kutokana na kutoa mimba japokuwa kufanya hivyo ni kosa kisheria, wengi hutoa.

 

Je dalili za tatizo lipo? Jibu ni kwamba tatizo hili halina dalili, mara nyingi wanawake wengi hubainika katika huduma za afya kuwa na tatizo hili pale wanapojikuta hawapati watoto na kufanyiwa uchunguzi.

VIPIMO NA UCHUNGUZI

Vipimo na uchunguzi vya tatizo hili ni pamoja na kipimo kinachojulikana kama Hysterosalpingography, kifupi HSG cha kuweka dawa maalum inayoingizwa katika nyumba ya uzazi na kusambaa katika mirija ya uzazi na kisha picha ya Xray hupigwa kuonesha tatizo.

 

Kipimo cha pili huwa ni cha Laparascopic ambacho chenyewe huwa na camera, taa na kisu na kifuko (angalia mchoro). Kifaa tiba hiki kinaweza kufanya kazi ya kuchunguza na kubaini tatizo na kukarabati na kuzibua mirija ya mayai iliyoziba hivyo mama kushika mimba.

 

USHAURI

Kwa wale wenye tatizo la kupata mimba ni vema wakafika kwenye kituo cha afya na kuonana na daktari ambaye baada ya uchunguzi atakushauri mgonjwa nini cha kufanya ili aweze kuzaa kama kawaida.

Comments are closed.