The House of Favourite Newspapers

Okwi: Nikipangwa Na Mghana Mtanikoma

0

 

Mshambuliaji wa kimataifa wa Simba, Mganda, Emmanuel Okwi.

MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Simba, Mganda, Emmanuel Okwi, juzi Jumamosi alimshuhudia mshambuliaji mwenzake wa klabu hiyo, Mghana, Nicholas Gyan katika mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Azam FC na akasisitiza jamaa huyo ni bonge la straika, sema tu watu hawajamshtukia.

Okwi alikuwa jukwaani katika mchezo huo na alishuhudia kila kitu kilichotokea.

Mganda huyo aliyetokea katika kikosi cha Ebusua Dwarfs, alishawahi kucheza na Gyan katika mchezo wa kirafiki kwenye Simba Day mwezi uliopita dhidi ya Rayon Sports ya Rwanda ambayo Simba ilishinda bao 1-0, halafu Mghana huyo akaondoka kumalizana na timu yake, tangu hapo hawakuwahi kukutana tena na Okwi, mpaka Mganda huyo alipomuona juzi, yeye akiwa jukwaani.

Mghana, Nicholas Gyan.

Okwi ambaye hakuitumikia Simba katika mchezo huo kutokana na kuchelewa kurudi nchini akitokea kwao Uganda alipokuwa ameenda kwa ajili ya kuitumikia timu yake ya taifa katika mchezo wa kuwania kufuzu kushiriki Fainali za Kombe la Dunia 2018 dhidi ya Misri, alisema anaamini akipangwa pamoja na Mghana huyo, safu ya ushambuliaji ya Wekundu haitakamatika.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Okwi alisema kuwa Gyan alionyesha uwezo mkubwa katika mchezo huo pamoja na John Bocco lakini walishindwa kufanya vizuri kutokana na kukamiwa na mabeki wa Azam.

 

“Gyan ni mchezaji mzuri, kuna vitu anavyo ambavyo naamini kuwa siku tukipangwa naye pamoja basi tutafanya makubwa kama yale tuliyofanya dhidi ya Ruvu Shooting tulipokuwa na Juma Liuzio.

“Lakini pia washambuliaji wengine katika kikosi chetu ni wazuri sana,” alisema Okwi.

 

Akizungumzia kuhusiana na kuchelewa kwake kurudi nchini kwa ajili ya kuitumikia timu hiyo katika mchezo huo uliomalizika bila ya kufungana, Okwi alisema: “Kilichonichelewesha kujiunga na timu yangu mapema ni kutokana na matatizo ya kifamilia lakini pia hali ya usafiri.

 

“Baada mechi yetu na Misri nilitakiwa kuja moja kwa moja Dar es Salaam lakini nilipata matatizo ya kifamilia ikanibidi niende kwanza nyumbani Uganda kisha ndiyo nije Dar.

 

“Hata hivyo, baada ya kuyatatua nilitakiwa nifike jana alfajiri (juzi) lakini kutokana na kubadilishwa kwa ratiba ya ndege niliyokuwa nije nayo, (Kenya Airways), nilijikuta nikichelewa kufika Dar jambo ambalo lilimfanya kocha pia ashindwe kunitumia katika mechi hiyo.

 

“Lakini pamoja na hali hiyo napenda kuwapongeza wachezaji wenzangu wote wa Simba kwa kazi kubwa waliyoifanya kwani mechi hiyo ilikuwa ni ngumu sana kwani Azam walipania sana,” alisema Okwi.

 

Okwi kwa sasa ndiye anayeongoza kwa kufumania nyavu katika mbio za kuwania kiatu cha dhahabu msimu huu akiwa na mabao manne ambayo yote kwa pamoja waliyafunga dhidi ya Ruvu Shooting ambapo Simba iliibuka na ushindi wa mabao 7-0.

Sweetbert Lukonge na Musa Mateja

Leave A Reply