The House of Favourite Newspapers

Pablo Awapa Majukumu Mazito Morrison, Sakho

0

KOCHA Mkuu wa Simba, Pablo Franco amesema amefurahishwa viwango vya mastaa wake hususani viungo, Pape Sakho na Bernard Morrison katika mchezo wao wa Jumapili iliyopita dhidi ya RS Berkane na anaamini nyota hao wataendelea kuwa na kiwango bora dhidi ya ASEC Mimosas, Jumapili hii.

 

Simba Jumapili iliyopita wakiwa katika Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar waliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Berkane katika mchezo wa hatua ya makundi Kombe la Shirikisho Afrika, ushindi huo umeifanya Simba kuongoza msimamo wa Kundi D wakiwa na alama saba.

 

Jumapili hii Simba inatarajiwa kushuka Stade de l’Amitie nchini Benin, kwa ajili ya mchezo wao wa tano dhidi ya ASEC Mimosas ya Ivory Coast. Mchezo huo unafanyika Benin kwa kuwa uwanja wa ASEC Mimosas nchini Ivory Coast uko kwenye marekebisho.

 

Katika mchezo huo, Sakho alifunga bao pekee la ushindi la Simba ambapo sasa anafikisha mabao mawili, huku Morrison ambaye mpaka sasa ana mabao matatu. Akizungumza na Championi Jumatano, Pablo aliwapongeza mastaa hao kutokana na msaada mkubwa ambao walionyesha kwenye mchezo dhidi ya Berkane.

 

“Nawapongeza sana wachezaji wangu kwa kupambana katika mchezo wetu wa Jumapili, nadhani kwa kiasi kikubwa walijitoa sana kuhakikisha tunapata matokeo, hususani Sakho aliyefunga bao na kina Morrison ambao waliingia kipindi cha pili na kuonyesha kiwango bora.

 

“Tuna mchezo mgumu wa ugenini Jumapili, ni mchezo ambao huenda ukatupa tiketi ya kufuzu robo fainali, hivyo natamani kuona wachezaji hawa wakiwa kwenye kiwango bora ili kuhakikisha tunapata matokeo,” alisema Pablo.

JOEL THOMAS NA LUNYAMADIZO MLYUKA Dar es Salaam

Leave A Reply