The House of Favourite Newspapers

Polisi Yatoa Ufafanuzi Sikukuu ya Pasaka

0

Jeshi la Polisi nchini Tanzania limesema halijazuia ibada za sikukuu ya Pasaka na kwamba walichozuia ni mikusanyiko, sherehe na makongamano ambayo yamekuwa yakifanyika katika sikukuu hiyo miaka ya nyuma.

 

 

Hayo yameelezwa leo Ijumaa Aprili 2, 2021 na msemaji wa jeshi hilo, David Misime katika mkutano na waandishi wa habari jijini Dodoma.

 

 

Jana Misime alitoa taarifa iliyoeleza kuwa polisi wamezuia shamrashamra za sikukuu hiyo kwa kuwa nchi ipo katika siku 21 za maombolezo ya kifo cha Rais wa awamu ya tano Hayati John Magufuli kilichotokea Machi 17, 2021.

 

 

Katika maelezo yake leo, Misime amesema taarifa inayosambaa katika mitandao ya kijamii kwamba polisi wamezuia ibada si kweli akisisitiza kuwa taarifa hizo zinalenga kupotosha umma na kuwachanganya waumini.

 

 

“Hata jana Alhamisi Kuu, Polisi wenye sare na waliovalia kiraia walikuwa kwenye doria kwa ajili ya kuimarisha ulinzi kwa wananchi ili wenye imani ya Kikristo waweze kwenda makanisani kuabudu kwa uhuru bila shaka,” amesema Misime.

 

 

Amefafanua kilichozuiwa ni sherehe ambazo zinakuwa na mikusanyiko mikubwa, “lakini watu wanapokuwa na familia zao katika matembezi ya kawaida hilo halijakatazwa wala watakaofanya mkusanyiko mdogo wa kifamilia majumbani mwao hawatahusika.”

Leave A Reply