TAARIFA zilizotolewa na Ikulu ya Marekani ‘White House’ zimeeleza kuwa, inaonekana kwamba wafungwa wote waliomo kizuizini katika Gereza la Guantanamo Bay wanatarajiwa kuachiliwa kabla rais Barack Obama hajaondoka rasmi madarakani mpaka kufikia Januari 20, 2017.
Rais Obama amesema kuifunga kambi hiyo ndiyo kipaumbele chake miaka nane iliyopita wakati alipokuwa akiingia madarakani. Akitilia mkazo maelezo hayo ameongeza kusema kwamba kuendelea kuwepo kwa gereza hilo kuna shusha hadhi ya Wamarekani.
Akiielezea kambi hiyo amesema kwamba imekuwa eneo la mashaka, kushikiliwa kwa muda mrefu, kulazimishwa kula chini ya ulinzi , kunyimwa usingizi, nafasi ya dhiki, vipigo visivyokwisha na kila aina ya mateso kwa wafungwa.
Mbali na hivyo idadi ya wafungwa imekuwa ikipungua kila kukicha huku mpango wa kuifunga kambi hiyo ya mateso umekuwa ukipingwa na Bunge la Congress.
Naye rais Mteule wa Marekani, Donald Trump ametanabahisha dhahiri msimamo wake na kupinga wazo la kumuachilia mfungwa yeyote kutoka katika gereza hilo.
Akiweka bayana msimamo huo kupitia mtandao wa kijamii wa twitter amesema kwamba wafungwa hao ni watu hatari na hawana ruhusa ya kurejea katika uwanja wa vita.
Comments are closed.