Zanzibar: Agosti 29, 2021: Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan mwishoni mwa wiki alikabidhiwa Kliniki inayohamishika (mobile Clinic) iliyotolewa na Benki ya NBC kwa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili kuboresha huduma ya afya hususani ya mama na mtoto visiwani humo sambamba na kuzindua jengo la madarasa ya skuli ya maandalizi ya Kizimkazi yaliyojengwa na kukarabatiwa kwa msaada wa benki hiyo.
Hafla ya uzinduzi na makabidhiano hayo ilifanyika Kijiji cha Kizimkazi Mkunguni Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar na kuhudhuriwa na baadhi ya viongozi waandamizi wa serikali ya Mapinduzi Zanzibar, akiwemo Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Wazee Jinsia na Watoto Zazibar, Ahmed Nassor Mazrui, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Katiba Sheria, Utumishi na Utawala Bora wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Haroun Ali Suleiman, Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja Rashid Hadid Rashid, viongozi wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC)na wananchi wa kijiji hicho.
Akizungumza wakati akizundua na kukagua jengo hilo pamoja na kliniki hiyo, Rais Samia aliishukuru benki hiyo kwa jitihada hizo huku akitoa wito kwa taasisi hiyo pamoja na taasisi nyingine za kifedha kuendelea kuunga mkono jitihada za serikali katika kuleta maendeleo kwa wananchi wake.
“Hongereni sana kwa jitihada hizi zinazowagusa wananchi moja kwa moja na zaidi naombeni sana muendelee kuiunga mkono serikali katika kuwaleta maendeleo wananchi katika maeneo yote,’’ alisema Rais Samia.
Awali akizungumza ofisini kwake wakati akipokea msaada wa vifaa tiba ikiwemo UtraSound machine vinakavyotumika kwenye kliniki hiyo, Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Wazee Jinsia na Watoto Zanzibar, Ahmed Nassor Mazrui pamoja na kuishukuru benki ya NBC kwa msaada huo, alisema serikali hiyo itahakikisha msaada huo unatumika kama ilivyokusudiwa.
“Msaada huu ni muhimu na unahitajika sana. Jukumu letu kama serikali ni kuhakikisha vifaa hivi vinatunzwa na vinatumika kama ilivyokusudiwa ili vilete tija iliyolengwa kwa maana visaidie haswa kuokoa maisha ya wazanzibar wakiwemo wakina mama na watoto hasa walipo pembezoni.
Aliahidi kwa niaba ya serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuendeleza ushirikiano na benki hiyo hususani kwenye masuala mbalimbali ikiwemo yale yanayohusu ustawi wa jamii huku akibainisha kuwa uimara wa benki hiyo kwenye utoaji wa huduma zake visiwani humo kwa kiasi kikubwa unachagizwa na namna inavyoshirikiana na jamii ya Wazanzibar ikiwemo kibiashara na mambo ya kijamii.
“Ndio maana naamini kabisa uimara wa benki ya NBC tangu ilipoanza kutoa huduma zake hapa Zanzibar ni matokeo ya ushirikiano iliyonayo na jamii ya Wazanzibar…nawapongeza sana na ninaomba muendelee kuguswa zaidi,’’ aliongezea.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC Bw Theobald Sabi alisema msaada huo wenye jumla ya thamani ya Tsh Milioni 275, ni muendelezo wa jitihada za benki hiyo za uwajibikaji kwa jamii (CSR)zinazosukumwa na dhamira kuu ya taasisi hiyo katika kushirikiana na jamii inayoihudumia.
“Benki ya NBC tumekuwa tukiguswa na changamoto mbalimbali zilizopo kwenye huduma za afya na elimu hapa nchini ikiwemo Zanzibar na ndio maana tumekuwa mstari wa mbele kuhakikisha tunashirikiana na serikali zote mbili kukabiliana na changamoto zinazohusu sekta hii muhimu.’’ Alisema huku akibainisha kuwa benki hiyo inaendelea kufanya jitihada zaidi ili kufanikisha misaada kama hiyo kwenye maeneo mengine ikiwemo visiwani Pemba.
Alisema huduma zitakazotolewa na kliniki hiyo kwa akina mama na watoto zitatolewa bure kwa kuwa zitagharamiwa na benki hiyo kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar .
“Pamoja na msaada huu benki ya NBC itaendelea kuhudumia vifaa vilivyopo ndani ya kliniki hii hata pale vitakapokuwa vinapata hitirafu za kiufundi. Tunaamini sasa kupitia huduma hii wataalamu wa afya wataweza kuwafikia walengwa popote walipo hususani wale waliopo pembezoni hususani wakina mama na watoto na kupitia msaada wa mwenyezi Mungu tutaweza kuokoa maisha yao,’’ aliongeza.
Mbali na ujenzi wa jengo la Madarasa katika wa skuli ya maandalizi Kizimkazi msaada huo pia umehusisha samani za ndani ya madarasa hayo ikiwemo madawati na meza sambamba na jiko kwa ajili ya upishi wa chakula cha wanafunzi hao pamoja na vifaa vya michezo ili kutoa fursa ya watoto kufurahia michezo yao.
Akizungumzia msaada huo wa Kliniki inayohamishika, Mratibu wa Huduma ya Afya ya Uzazi na Mtoto, Wizara ya Afya Zanzibar Bi Wanu Bakari alisema msaada huo umefika wakati muafaka kwa kuwa serikali hiyo inapambana kusogeza huduma za afya hususani maeneo ya pembezoni ili kuepukana na changamoto ya vifo vya akina mama na watoto wakati wa kujifungua.
“Tunaishukuru sana benki ya NBC kwa kuliona hili na kwa kweli wametugusa sana! Kwa mfano kupitia kliniki hii tutaweza kutoa huduma ya Utrasound ambayo ni muhimu sana. Kwa kwasasa tunakabiliwa na uhaba wa huduma hii hivyo kupitia msaada huu tatizo linakwenda kupungua.’’
“Zaidi pia miongoni mwa vifaa vitakavyokuwemo kwenye kliniki hii pia ni vifaa vya uchunguzi wa afya za kina mama wajawazito kitu ambacho kitatusaidia kuwafanyia uchunguzi kwa haraka pale itakapohitajika na kabla hawajapata madhara zaidi,’’ aliongezea.