Rais Samia Apokea Taarifa Ya CAG Na Takukuru – Ikulu, Dar Es Salaam – (Picha +Video)
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akipokea ripoti ya taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na TAKUKURU kwa mwaka 2021/2022 leo Machi 29, 2023 Ikulu jijini Dar es Salaam
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere amesema mpaka kufikia Juni 30, 2022 deni la serikali lilikuwa Sh tril 71.31 ikilinganishwa na Sh tril 64.52 mwaka 2020/2021, ikiwa ni ongezekezo la Sh tril 6.79 sawa na asilimia 10. 5 ikilinganisha na Sh tril 7.79 sawa na asilimia 13.7 kwa mwaka uliopita.
CAG Kichere amesema wakati akitoa taarifa kuhusu uwasilishaji wa ripoti ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali kwa mwaka wa fedha ulioishia 30 Juni, 2022 katika Ikulu ya Dar es Salaam.
Akiwasilisha taarifa hiyo, CAG Kichere amesema kuwa deni la ndani limefikia Sh tril 24.04 na deni la nje Sh tril 47.27 kwa mwaka wa fedha 2021/2022. Mwaka wa fedha 2020/ 2021 deni la ndani lilikuwa Sh tril 18.93 ndani na nje Sh tril 45.79.
Wakusanyaji wa mapato katika mamlaka 98 za serikali za mitaa hawakuwasilisha Sh bilioni 11.07 katika akaunti husika za benki. Hii ni kwa mujibu wa ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere.
Akiwasilisha ripoti hiyo, CAG Charles Kichere amesema suala hilo limetokana na ufuatiliaji duni na kutofanya upatanisho wa hesabu za mara kwa mara.
Ripoti hiyo imeeleza kuwa wakala wa ukusanyaji wa mapato katika mamlaka 10 za serikali za mitaa, hawakuwasilisha Sh bilioni 4.12 kwenye benki.
Aidha, CAG Charles Kichere amewashauri wakurugenzi wa mamlaka za serikali za mitaa kuhakikisha fedha zote ambazo hazikuwekwa benki zinawekwa kwa kufuata sheria za ukusanyaji wa mapato ya serikali.