The House of Favourite Newspapers

Aussems: Tutawachapa Mazembe kwao

KOCHA Mkuu wa Simba, Patrick Aussems, amefunguka kuwa licha ya kutoka sare katika mchezo wao wa juzi wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya TP Mazembe, ana matumaini makubwa ya kutinga nusu fainali.

 

Simba ilitoka suluhu katika mechi yake na Mazembe ya robo fainali iliyochezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, lakini John Bocco alikosa penalti huku Meddie Kagere akigongesha mwamba.

Simba wanatarajia kurudiana na Mazembe Jumamosi hii nchini DR Congo mchezo ambao unaonekana kuwa na upinzani mkubwa.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Aussems alisema kuwa ameridhishwa na kiwango cha wachezaji wake jinsi walivyocheza katika mchezo huo, hivyo ana uhakika atafanya vyema katika mchezo wa marudiano na anajipa matumaini ya kutinga nusu fainali.

 

“Nimefurahishwa na kikosi changu, japokuwa tumepoteza nafasi nyingi za wazi ambazo tulitakiwa kufunga, nakiandaa kikosi changu kwa ajili ya mchezo wa marudiano na nina matumaini tutashinda na kuingia nusu fainali.

 

“Nafanyia kazi makosa yaliyojitokeza ili kuweza kuimarisha kikosi changu kabla ya mchezo wa marudiano.

“Maamuzi ya mwamuzi hayakuwa mabaya, alifanya kile ambacho alikiona kinastahili yeye kama mtu yeyote anaweza kufanya makosa na hata mimi kocha naweza kuwa na upungufu wangu,” alisema Aussems.

KHADIJA MNGWAI, | Dar es Salaam

Comments are closed.