The House of Favourite Newspapers

Samatta: Kweli Naenda Kucheza England


Sweetbert Lukonge | CHAMPIONI JUMAMOSI  | Dar es Salaam

STRAIKA wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Samatta, amesema anapenda kucheza soka katika Ligi Kuu England ambako anavutiwa na uchezaji wa kiungo wa Chelsea, Eden Hazard.

Samatta ambaye kwa sasa anakitumikia kikosi cha KRC Genk cha Ubelgiji, hivi karibuni amekuwa na kiwango cha hali ya juu kilichozifanya timu nyingi za Ulaya kumtolea macho.

Hivi karibuni baba wa straika huyo, Ally Pazi Samatta, alisema mwanaye huyo angependa kwenda kucheza England kwa kuwa ndiyo ndoto yake ya muda mrefu kucheza huko.

Akizungumza na Championi Jumamosi, Samatta alisema ni mapema mno kusema timu gani zinazomuwania kwa sasa, bali lengo lake siku moja kwenda kucheza soka England.

“Malengo yangu siku moja ni kwenda kucheza soka katika Nchi ya England japo kwa sasa timu nyingi zimeonyesha nia ya kunihitaji. Zipo timu za ndani na nje ya Ubelgiji, inavyoonekana zinasubiri mpaka kipindi kijacho cha usajili kifike ili waanze mchakato huo.

“Zamani nilivyokuwa mdogo, nilikuwa navutiwa na uchezaji wa Mussa Hassan Mgosi ambaye ndiye aliyenifanya mpaka leo hii kuwa mshambuliaji mahiri, lakini hivi sasa navutiwa na uchezaji wa Eden Hazard,” alisema Samatta.

Samatta leo Jumamosi ataiongoza Taifa Stars kucheza mechi ya kirafiki dhidi ya Botswana kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Comments are closed.