The House of Favourite Newspapers

Simba SC Wataja Mechi Za Ubingwa

Kikosi cha Timu ya Simba kikiendelea na mazoezi.

KOCHA Msaidizi wa Simba, Mrundi, Masoud Djuma, ametamka kuwa kama timu yao ikifanikiwa kupata ushindi kwenye mechi ngumu saba muhimu ikiwemo dhidi ya Yanga, basi wataomba wapewe kombe lao la Ligi Kuu Bara. Kauli hiyo, aliitoa mara baada ya kuwafunga Azam FC, juzi Jumatano kwenye mechi ya ligi iliyochezwa katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Mechi hiyo ilikuwa na ushindani mkubwa kwa kila timu kutokana na kila moja kuhitaji pointi tatu ili iweze kuchukua pointi tatu na kujiwekea mazingira mazuri ya ubingwa wa ligi.

 

Akizungumza na Championi Ijumaa, Djuma alisema wao benchi lao la ufundi chini ya Kocha Mkuu Mfaransa, Pierre Lechantre kabla ya kuanza mzunguko wa pili waliweka mikakati ya kushinda michezo saba migumu ili wawaache wapinzani wao Azam na Yanga kwa idadi kubwa la pointi. Djuma alisema wameanza kuona malengo yao yakianza kutimia kwa kuwafunga Azam wanaofukuzana kileleni wakiwa na pointi 33 chini ya Yanga wenye 34.

 

Aliongeza kuwa, mechi hizo walizopanga kushinda ni dhidi ya Yanga, Singida United, Mtibwa Sugar, Tanzania Prisons, Mbao FC, Lipuli FC na Azam ambao tayari wamewafunga bao 1-0 ambalo limefungwa na Mganda, Emmanuel Okwi. “Kama unavyofahamu hivi sasa Simba imebakisha kombe moja pekee la ligi kuu baada ya kuondolewa kwenye Kombe la FA na kulikosa Kombe la Mapinduzi.

 

“Malengo yetu ni kuchukua ubingwa huu na hilo linawezekana kutokana na ubora wa kikosi chetu ambacho kila siku tunaendelea kukiimarisha ili tufikie malengo yetu,” alisema Djuma.

Comments are closed.