Simba Wakwepa Hujuma za Waarabu
UONGOZI wa Klabu ya Simba umefunguka kuwa umejipanga kikamilifu kuhakikisha wanazikwepa hujuma zote ambazo watafanyiwa na wapinzani wao Al Masry mara watakapoingia nchini Misri kwa ajili ya kwenda kuvaana na klabu hiyo.
Simba wanatarajiwa kukwea pipa na kuwafuata Al Masry keshokutwa Jumatano kwa ajili ya kwenda kurudiana nao kwenye mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika baada ya kucheza nao jijini Dar na kutoka nao sare ya mabao 2-2.
Akizungumza na Championi Jumatatu, Kaimu wa Simba, Salim Abdallah ‘Try Again’ amesema kwamba wanajua safari yao ya Misri itakuwa na hujuma na figisu nyingi kutoka kwa wapinzani wao kwa ajili ya kuwatoa kwenye akili ya mchezo lakini wao wamejipanga kukabiliana na jambo hilo ili kutimiza lengo la kuwaondosha Waarabu hao kwenye michuano hiyo.
“Sisi kama viongozi tunajipanga vilivyo kuhakikisha kwamba mchezo ujao tunafanya vyema na kusonga mbele, tunajua kwamba wapinzani wetu wakiwa kwao wanakuwa na hujuma nyingi sana nje ya uwanja za hapa na pale kwa ajili ya kuwaondoa tu msiwe na mawazo ya mechi, lakini tunajipanga kikamilifu kuhakikisha kwamba tunapambana nazo.
“Kwa mikakati ambayo tunaendelea kuiweka tunaamini kwamba tutafanya jambo kubwa kwa kuwasukuma nje wapinzani wetu tukiwa hukohuko ugenini na jambo hilo linawezekana kwa sababu sisi kama uongozi tunatimiza majukumu yetu kwa asilimia zote kuiandaa timu kwa ajili ya mchezo huo muhimu,” alisema Try Again.
Simba wanaofundishwa na Mfaransa Pierre Lechantre watarudiana na Al Masry Machi 17, mwaka huu nchini Misri ukiwa ni mchezo wa mkondo wa pili wa kombe hilo la Shirikisho.
Said All, Dar es Salaam
Comments are closed.