SIRI DIRECTOR CAMPOS KUIVURUGA BONGO
WAKATI madairekta wa video za muziki Bongo wakiwa wamelala, wanamuziki wameamka na wanataka kazi zao zipae mbali zaidi wakikimbilia bondeni kwa Madiba yaani Afrika Kusini na wengine Nigeria ili kutengeneza kazi bora za kuwatangaza kimataifa.
Miongoni mwa majina ya mwanzo kabisa ya madairekta waliofanya kazi na wanamuziki hao ni Godfather kutoka Afrika Kusini, ambaye alifanya video ya wimbo wa Mwana wa Alikiba na Nana wa Diamond ambao alimshirikisha Mr Flavour.
Hizo ndizo baadhi ya nyimbo zilizompa umaarufu nchini Godfather. Lakini kadiri muda ulivyokwenda mbele wanamuziki hao kutoka Bongo waligundua chimbo lingine la jamaa anayetengeneza video kali aitwaye Justin Compas, mmiliki wa Kampuni ya Gorilla Film.
Huyu akawa ni kimbilio la wanamuziki wengi wa Bongo na kiukweli amefanya kazi nyingi na wanamuziki pamoja na madairekta wa hapa nchini.
Justin ambaye kwa upande wa kimataifa ametengeneza video kali ikiwemo New Guy ya mwanamuziki Sarkodie ambayo alimshirikisha mwanamuziki kutoka Marekani, Ace Hood, KibongoBongo amefanya video nyingi zikiwemo No Body But Me ya Vee Money na KO, Game ya Navy Kenzo, One More Night ya Jux, Don’t Bother ya Joh Makini aliyomshirikisha A.K.A na Toba ya Shaa.
Lakini pia baadhi ya madairekta ambao ameshirikiana nao ni pamoja na Hanscana, Khalfani Alimendro pamoja na Msafiri.Sasa wengi wanaweza kuwa wanajiuliza ni kwa nini dairekta huyu amefanikiwa kufanya kazi na wanamuziki wengi Bongo hata kuivuruga Bongo kama huko kwao Afrika Kusini?
Tena kwa kiasi cha kufika maeneo mengi yakiwemo Mbagala alikoshutia Wimbo wa Wet wa Vee Money na G Nako, ambao ni wimbo namba tisa kwenye albamu ya Money Mondays Tandale,Zanzibar na maeneo mengine mengi siri ni hii hapa;
Kwa nyakati tofauti Uwazi Showbiz, imezungumza na wanamuziki tofautitofauti pamoja na madairekta ambao wameweka wazi kwamba jamaa huyu mbali na kutengeneza video kali lakini ni dairekta anayeipenda Bongo na anaukubali sana muziki wa Bongo. Msikie Vee Money ambaye ametoka kufanya naye kazi hivi karibuni wakishuti video ya wimbo wa Wet;
“Compas kiukweli anajua anachokifanya. Ninapenda kufanya naye kazi kwa sababu mnapofanya kazi anafanya kwa moyo na furaha akitaka kile kinachofanyika kitoke bora.
“Lakini pia anapenda muziki wa Bongo na namna tunavyofanya kazi, kwa hiyo ndiyo maana anakuwa mwepesi unapomtafuta kufanya naye kazi.”
Kwa upande wa Joh Makini akizungumza na Uwazi Showbiz, alisema; “Ni vigumu kushindana bei na Compas unapodhamiria kufanya naye kazi. Hayupo juu sana, maongezi ukiyaweka naye vizuri, ukiwa na kazi nzuri unaweza kumtoa Afrika Kusini na kumleta Bongo ili ufanye naye kazi.”
Kwa upande wake, dairekta Hanscana ambaye amewahi kufanya kazi na dairekta huyu, naye alikuwa na haya ya kusema;
“Compas ni mwalimu, dokta wa video na mtu ambaye anapenda kugawa kile anachokifahamu na kujifunza vitu vipya kutoka kwa watu wengine.
“Ndiyo maana akija Bongo atapenda kukutana na madairekta wa Bongo anapokuwa anataka kufanya kazi yake ili wamsaidie katika mambo kadha wa kadha kwani wao wanapajua zaidi Bongo. Binafsi ndiyo siri kubwa ya kufanya naye kazi, kujifunza kutoka kwake.”
Hizo ndizo baadhi ya siri zinazomfanya dairekta huyu kupiga kazi na wanamuziki pamoja na madairekta wengi kutoka Bongo. Wengi wameonekana pia kujifunza mengi kutoka kwake, hata kufanya kazi bora na kupunguza lindi la wanamuziki kukimbilia Sauz kwa ajili ya kushuti video.
Comments are closed.