The House of Favourite Newspapers

SIRI YA TAMBIKO LA WAZIRI KIGWANGALLA YAFICHUKA

Dk. Hamisi Kigwangalla

SIRI ya Waziri wa Maliasili na Utalii ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Nzega Vijijini la mkoani Tabora, Dk. Hamisi Kigwangalla kufanyiwa tambilo la kimila jimboni kwake imefichuka.

Hivi karibuni wazee wa mila na watemi wakiongoza na Chifu Ng’wana Ng’washi wa Wasukuma walifanya tam­biko la kichifu la kumtambikia ili akawe tayari kwa kazi za kulitumikia taifa katika maju­kumu ya kibunge na uwaziri.

Akizungumza na gazeti hili, Kigwangalla amesema hawezi kuacha mila hiyo na wakati akifanyiwa hayo ali­washukuru viongozi mbalim­bali wa dini nchini kwa dua na maombi yao kwa kipindi chote alichopata ajali hadi sasa kupona na kure­jea tena na majukumu yake.

Aidha, alitoa siri kwa kuwaambia wananchi wa jimbo lake kuondoa hofu licha ya kuwepo watu waliokuwa wak­ipitapita jimboni kwa lengo la kulinyemelea na kutoa maneno ya kumkatisha tamaa.

“Kwa waliokuwa wanatembea na wakikesha usiku kucha wakisubiri nife wameanguka. Mungu amesimama mbele yangu, mimi ni mzima naendelea kutekeleza majukumu yangu mdogomdogo mpaka nitakapokuwa imara kabisa na sasa naanza upya.

“Kwa sasa nime­anza kurudi kwenye majukumu yangu kama kawaida. Kwa hivyo nikaona kabla ya kuanza kuoneka­na nikiruka huku na kule kwenye maju­kumu ya kiwizara, nikasema hapana, nirudi kwanza ny­umbani nipate dua za wazazi wangu, dua za wazee na viongozi wa dini.

“Kwa tukio lile (la ajali) kwa sisi tunaoamini, ni mkono wa Mungu ulikuwa mahala pale,” alisema Dk. Kigwangalla.

Aliongeza kuwa amefanya mkutano wake wa pili uliofan­yika katika Kata ya Lusu, Tarafa ya Nya­sa iliyopo kwenye jimbo lake hilo la Nzega Vijijini, hivi karibuni, na amewashukuru viongozi wa dini pamoja na wazee wa mila kwani wao wamekuwa chachu kwenye kupona kwake tokea alipolazwa hospitali kwa zaidi ya miezi miwili kwa kuuguza majeraha ya mwili wake kuto­kana na ajali ya gari aliyopata Agosti 4, mwaka huu.

Alisema viongozi wa hao wa dini na wa kimila pamoja na wananchi kila mmoja kwa nafasi yake walikuwa ni wa kipekee na dua zao zimeweza kusaidia na kwa sasa amerejea kutoa shukrani na kupokea dua zao hizo kwani kwa sasa ameanza kufanya kazi.

Dk. Kigwangalla yupo katika ziara ya kutoa shukrani na dua maalum kwa wananchi wa jimbo lake hii ni tokea kurejea kutoka kuuguza majeraha ya mwili baada ya kupata ajali Agosti 4, mwaka huu wakati akiwa katika majukumu yake ya kikazi mkoani Manyara

Comments are closed.