WAZIRI wa Maliasili na Utalii Profesa Jumanne Magembe amewapongeza waandishi wa habari kwa mchango wao kuendelea kutangaza utalii nchinikupitia vyombo vyao, na kuwaomba waendelee na uzalendo huo kwani kitendo hicho ni faida kwa taifa zima.
Pongezi hiyo ameitoa leo jijini Tanga alipokuwa akifungua semina ya mwaka kwa wahariri na wanahabari waandamizi iliyoandaliwa na Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (TANAPA).
Waziri Magembe amesema matokeo ya wanahabari kutumia kalamu zao kutangaza utalii yanajionesha wazi kwa ongezeko la idadi ya watalii kutoka nchi mbalimbali kutembelea hifadhi zetu.
Aidha ameitaka TANAPA kuendelea kushirikiana na wanahabari kwa kufanya semina hizo kila mwaka ili kupata mrejesho juu ya kazi wanayoifanya, kwani vyombo vya habari ni fursa nzuri ya kutoa elimu kwa umma na kutangaza shughuli mbalimbali zinazofanywa na mamlaka hiyo.
Mkutano huo wa siku tatu ulioanza leo Julai 26 unatarajia kumalizika Julai 29, ambapo wanahabari watajifunza na kujadiliana masuala mbalimbali ya utalii na uhifadhi.