The House of Favourite Newspapers

Thamani Women Tanzania, Simba, Azam na Singida FG Waungana Kupinga Ukatili Dhidi ya Wanawake, Watoto

0

 

Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Khamis Mwinjuma “ Mwana FA) (wa pili kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Afisa Mtendaji Mkuu wa Simba, Imani Kajula (wa kwanza kulia),Mkurugenzi mtendaji wa taasisi ya Thamani Women Tanzania Nafue Nyange (wa tatu kulia), Waziri Mkuu Mstaafu John Malecela (wa tatu kushoto), Afisa Mtendaji Mkuu wa klabu ya Azam FC, Abdulkarim Popat (wa pili kushoto) na Afisa Mtendaji Mkuu wa klabu ya Singida Fountain Gate, Olebile Sikwane wakati wa uzinduzi wa kampeni maalum ya kupinga ukatili dhidi ya wanawake na watoto ijulikanayo kwa jina la Piga Mpira, Sio Mwanamke.

Shirika lisilo la kiserikali (NGO), Thamani Women Tanzania, imezindua kampeni yake ya kwanza ijulikanayo kwa kauli mbiu ya ‘Piga Mpira Sio Mwanamke’ yenye lengo la kukemea na kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto nchini Tanzania.

Uzinduzi huo umefanyika katika Hoteli ya Hyatt, Regency kwa kushirikiana na timu za soka za Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Simba SC, Azam FC na Singida Fountain Gate na kuzinduliwa na Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Khamis Mwinjuma (FA).

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mkurugenzi Mkuu wa Thamani Women Tanzania, Nafue Nyange alisema kuwa taasisi hiyo iliamua kutumia mpira wa miguu kwa lengo la kufikisha haraka na kwa kishindo ujumbe wao kwani mashabiki wa mpira wa miguu kwa idadi kubwa zaidi ni wanaume wa makamo na matabaka tofauti.

Nyange alisema kuwa wachezaji wa timu hizo ambao watarekodi sauti na video za kupinga vitendo kikatili na kusambazwa katika mitandao ya kijamii, redio na wanaamini kuwa jamii itafikiwa kwa haraka na kukomesha kabisa janga hili.

Mkurugenzi mtedaji wa taasisi ya Thamani Women Tanzania Nafue Nyange akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni maalum ya kupinga ukatili dhidi ya wanawake na watoto ijulikanayo kwa jina la Piga Mpira, Sio Mwanamke.

“Wanamichezo wana fadhila na majukumu kwa mashabiki wao. Hakuna michezo bila mashabiki…lakini pia hakuna mashabiki bila amani na upendo katika jamii. Mashabiki tunawaazima wanamichezo sauti zetu kwa shauku kubwa katika kushangilia ligi zenu mbalimbali hivyo wanamichezo hamna budi kutu-azima mashabiki sauti zenu katika kupinga ukatili na majanga mengine ya jamii,” alisema Nyange.

Alifafanua kuwa kwa kuanzia, wamechagua timu hizo tatu ambapo baadaye watatanua wigo kwa kushirikisha timu nyingine pale tu watakapokuwa tayari kujiunga nao.

Kwa mujibu wa Nyange, kampeni hiyo itaanzia kwenye mikoa minne ya Mara, Mwanza, Dodoma na Dar es Salaam. Alisema kuwa kampeni hiyo pia itatambulishwa rasmi mikoa tofauti kwa awamu. Alisema kuwa takwimu zinaonyesha kuwa mikoa hiyo ina vitendo vingi viovu dhidi ya wanawake na watoto.

Aliongeza kusema kuwa watatumia njia mbalimbali kufikisha ujembe huo ikiwa pamoja na mechi za kirafiki, matukio ya jamii, na shughuli za elimu.

“Kampeni hii inalenga kutoa maarifa kuhusu madhara ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto, na pia kuchochea mazungumzo kuhusu jinsi ya kuzuia na kukomesha vitendo hivyo visivyo vya kibinadamu. Tunakaribisha kushiriki katika kampeni hiyo muhimu, tunaamini kupitia umoja wetu, tunaweza kuleta mabadiliko katika jamii yetu na kuwahakikishia wanawake na watoto ulinzi wanayostahili,” alisema.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Khamis Mwinjuma ambaye alikuwa mgeni rasmi, alivipongeza vilabu hivyo na kutoa rai kwa vilabu vingine vya mpira wa miguu kuunga mkono kampeni hiyo.

Mkurugenzi mtedaji wa taasisi ya Thamani Women Tanzania Nafue Nyange akizungumza wakati wa uzinduzi wa kampeni maalum ya kupinga ukatili dhidi ya wanawake na watoto ijulikanayo kwa jina la Piga Mpira, Sio Mwanamke.

Naibu Waziri alisema kuwa mpira wa miguu ni mchezo namba moja nchini na una mashabiki wengi na kama wachezaji na viongozi watashiriki katika kampeni za kupinga ukatili kwa wanawake na watoto, jamii itabadilika na kuwa na fikra chanya.

“Ni wakati wa kutumia nafasi zetu kuunga mkono kampeni hizi ili jamii ibadilike, wachezaji na viongozi ni kioo cha jamii na wote tukiungana, tutafikia malengo yetu,” alisema Mwinjuma.

Aliongeza kwa kusema kuwa: “Vita ya ukatili ni yetu sote, usalama na furaha ya wanawake na watoto ndio chanzo cha maendeleo na amani ya sasa na kesho. Nichukue nafasi hii kuviomba vilabu vingine vya mpira wa miguu kujiunga na kampeni hii ya Piga Mpira Siyo Mwanamke. Tuunge mkono bidii za serikali ya awamu ya sita na taasisi ya Thamani Women Tanzania kwa mpango wake mahusisi wa kuondoa janga hili,”.

“Ni lazima vijana wa kiume watambue ya kwamba katika janga hili wao ni suluhu na sio tatizo tu kwa hivyo ni muhimu wajadili tatizo hili,” alisema.

Kwa upande wake, Neema Tarimo ambaye ni Meneja Mradi wa Thamani Women Tanzania alisema kuwa wamejipga vilivyo kufikisha ujumbe na kuhakikisha kuwa kampeni hii inakamilika.

“Nachukua fursa hii kuwapongeza viongozi wa timu hizi tatu na wadau kwa kutuunga mkono katika kampeni hii muhimu kwa ustawi wa jamii, tunaamini tutafanikiwa,Tunakaribisha kushiriki katika kampeni hiyo muhimu, tunaamini kupitia umoja wetu, tunaweza kuleta mabadiliko katika jamii yetu na kuwahakikishia wanawake na watoto ulinzi wanayostahili,” alisema Tarimo.

Tarimo alifafanua kuwa kwa kwa njia ya mechi za kirafiki, matukio ya mbalimbali ya kijamii, na shughuli za elimu, kampeni hii inalenga kutoa maarifa kuhusu madhara ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto, na pia kuchochea mazungumzo kuhusu jinsi ya kuzuia na kukomesha vitendo hivyo visivyo vya kibinadamu.

Wakati huo huo Mtendaji Mkuu wa Simba, Imani Kajula alisema watatumia wachezaji wao na mitandao ya kijamii kupinga ukatili wa wanawake na watoto kwa nguvu zote.

Kauli hiyo iliungwa mkono na Ofisa Mtendaji Mkuu wa timu ya Azam FC, Abdulkarim Popat na wa Singida Fountain Gates FC, Olebile Sikwane.

Leave A Reply