The House of Favourite Newspapers

TMA Yatabiri Upungufu wa Mvua

0

MAMLAKA ya Hali ya Hewa nchini (TMA) imetoa ushauri wa mvua za vuli na kusema kuwa maeneo mengi nchini yatakuwa na mvua kidogo zitakazoambatana na vipindi virefu vya ukavu katika maeneo mengi ya nchi.

 

Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk. Agnes Kijazi ameyasema hayo leo Septemba 8, 2020 jijini Dar es Salaam wakati akitoa mwelekeo wa msimu wa mvua hizo za Oktoba hadi Desemba, 2020 ambazo ni mahususi katika maeneo yanayooata mvua mara mbili kwa mwaka.

 

Amesema, maeneo hayo ambayo ni Nyanda za juu Kaskazini-Mashariki, pwani ya Kaskazini pamoja na Visiwa vya Unguja na Pemba, Ukanda wa ziwa Victoria pamoja na kaskazini mwa Mikoa ya Kigoma na Morogoro yanatarajiwa kuwa na mvua chini ya wastani hadi wastani.

 

Maeneo mengi ya ukanda wa Ziwa Victoria, nyanda za juu kaskazini mashariki, pwani ya Kaskazini pamoja na maeneo ya kaskazini mwa mkoa wa Kigoma (wilaya ya Kibondo, Kakonko na Kasulu) yanatarajiwa kuwa na mvua za chini ya wastani hadi wastani.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya hali ya hewa TMA, Dkt. Agnes Kijazi, akitoa taarifa ya uelekeo wa mvua za vuli kwa kipindi cha Oktoba hadi Desemba, 2020, katika ofisi za mamlaka hiyo zilizopo Ubungo jijini Dar es Salaam. Kushoto kwake ni Meneja wa kituo cha utabiri TMA, Samwel Mbuya.

Mvua za vuli katika maeneo ya nyanda za juu kaskazini mashariki, na Ukanda wa Pwani ya Kaskazini pamoja na kaskazini mwa mkoa wa Morogoro zinatarajiwa kuanza kunyesha kwa kuchelewa kati ya wiki ya pili na ya tatu ya mwezi Novemba, 2020.

 

Dkt. Kijazi amesema pia mvua hizo zinatarajiwa kuanza wiki ya pili ya mwezi Septemba 2020 katika mkoa wa Kagera na kutawanyika katika mikoa ya Mwanza, Geita, Mara, Simiyu, Shinyanga na Kaskazini mwa mkoa wa Kigoma katika wiki ya tatu ya mwezi Septemba na zinatarajiwa kuisha Januari mwaka 2021.

 

Aidha maeneo ya ukanda wa Pwani ya Kaskazini, mikoa ya Dar es Salaam, Tanga, Pwani, Visiwa vya Sungura na Pemba pamoja na Kaskazini mwa mkoa wa Morogoro mvua zinatarajiwa kuwa chini ya wastani hadi wastani na zinatarajiwa kuanza kwa kuchelewa katika wiki ya pili na ya tatu ya mwezi Novemba,2020 na kuisha katika wiki ya nne ya mwezi Disemba.

 

Amesema kuwa, kutokana na mvua hizo kuwa kidogo athari mbali mbali zinaweza kujitokeza ikiwemo upungufu wa unyevunyevu katika udongo na hivyo, uwezekano wa kutokea moto maporini na kwenye misitu pamoja na upungufu wa maji safi na salama.

Mchambuzi wa hali ha hewa, Veronica Mgarula, akisoma utabiri.

“Tunatarajia kwamba kutakuwa na upungufu wa unyevunyevu katika udongo hivyo sekta husika inaweza kuangalia ni namna gani wanaweza kujiandaa vizuri kwa ajili ya kukabiliana na visumbufu vya mazao na magonjwa mbalimbali ambayo yanajitokeza na ambayo yanatarajiwa kuongezeka.

 

Aidha Dk. Kijazi amewashauri wakulima kutumia utabiri huo kwa kupanda mbegu na mazao yanayoweza kukomaa ndani ya muda mfupi huku pia mbinu na teknolojia za kilimo himilivu za kuhifadhi unyevunyevu na maji zikishauriwa kutumika.

 

Pamoja na hayo Dkt. Kijazi amesema kutokana na utabiri huo sekta ya usafirishaji zinatarajiwa kunufaika hususani katika usafiri wa anga na nchi kavu hivyo ni vema sekta husika wakautumia muda huu kuimarisha ujenzi wa miundombinu ya usafirishaji hasa kanye maeneo yanatokea mafuriko.

Leave A Reply