Video: Tundu Lissu Afungukia Hukumu ya Lijualikali, Aahidi Kumtetea
Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (pichani mwenye kofia) ambaye pia ni Mwanasheria Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), amesema hukumu aliyopewa Mbunge wa Kilombero kwa tiketi ya chama hicho, Peter Lijualikali, ni ya kisiasa na ilipangwa na chama cha mapinduzi kwa ajili ya kuikomoa Chadema lakini akaahidi kufanya kila linalowezekana, kuhakikisha anamtetea mbunge huyo mahakamani kwa kukata rufaa.
Akizungumza na waandishi wa habari leo kwenye makao makuu ya chama hicho, Kinondoni jijini Dar es Salaam, Lissu alisema Chadema inaamini Lijualikali ni mfungwa wa kisiasa na kwamba adhabu ya kifungo bila faini, ni kinyume na haki za binadamu na imetolewa kisiasa.
“Kwanza walimshitaki mheshimiwa Lijualikali mara mbili wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu ili wamfunge asiweze kuendelea na kampeni, haikuwezekana kumfunga na mwisho alishinda ubunge wa Jimbo la Kilombero kwa kishindo, baadaye walimfungulia kesi Mahakama Kuu ambako nako tuliwashinda vibaya… tayari timu ya wanasheria wa chama imeshaanza taratibu za kukata rufaa na maombi ya dhamana ya dharura wakati uamuzi juu ya rufaa yake unasubiriwa, tunatarajia kukamilisha taratibu hizi hadi kufikia Jumatatu ijayo.
Mbunge wa Kilombero kwa tiketi ya chama hicho, Peter Lijualikali
Lissu aliendelea kueleza kuwa, kisheria, hata kama mbunge huyo atatumikia kifungo hicho, hataweza kuvuliwa ubunge wake kwa sababu sheria inaeleza kuwa mtu atakayevuliwa ubunge, ni aliyetumikia kifungo cha zaidi ya miezi sita na kwamba kosa alilolifanya, siyo la utovu wa uaminifu kama katiba inavyoeleza.
Denis Mtima/ GPL
Comments are closed.