The House of Favourite Newspapers

Umoja Wa India Na Tanzania Waandaa Mbio Za Riadha

0

UMOJA wa nchi za India na Tanzania wameandaa mbio za riadha zitakazofanyika Desemba 30 na 31 jijini Dar es Salaam.

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Balozi wa India nchini, Binaya Srikanta Pradhan, alisema mbio hizo zitahusisha wakimbia ambao ni raia wa Tanzania na India.

Alisema wameandaa mbio hizo kuhakikisha wanadumisha umoja uliopo kati ya nchi hizo mbili ikiwemo wanariadha mbalimbali kubadilishana mawazo.

Alisisitiza kuwa mbio hizo pia zitahudhuriwa na mwanariadha mkongwe na Balozi wa Fit India, Milind Soman, ambaye alishaibua vipaji mbalimbali vya mchezo huo kuanzia hatua ya mitaa huko Mumbai, India.

Aliongeza Soman ambaye kwa sasa ni mkufunzi wa mbio za riadha nchini India, atapata fursa ya kuzungumza na wanariadha mbalimbali kuhakikisha wanabadilishana uzoefu.

Alisema mbio hizo siku ya kwanza zitaanzia mitaa ya Dar es Salaam hadi Bagamoyo na siku ya pili zitaanzia Bagamoyo kurudi Dar es Salaam ambapo zitajumusha kilometa 120.

“Umoja wa India na Tanzania tumeandaa mbio za riadha ambazo zitafanyika kuanzia Dar es Salaam hadi Bagamoyo mkoani Pwani na baadaye zitatoka Bagamoyo kurudi Dar es Salaam ambapo tutakimbia kilometa 120, pia tutakuwa na mkongwe Soman ambaye hivi sasa ni mkufunzi wa mchezo na msanii wa filamu nchini India,” alisema Balozi wa India nchini, Pradhan.

Naye Soman aliongeza: “Ni fursa nzuri kwetu kutembelea Tanzania kuja kuiongoza timu itakayoshiriki mbio za riadha kwa pamoja ambapo tutaungana na Watanzania mbalimbali lengo ikiwa ni kubadilishana uzoefu.

“Nimeshafanya safari kama hizi katika nchi mbalimbali ulimwenguni, sasa ni zamu ya Tanzania, kuhakikisha tunafikia malengo.

“Tunafurahi na tunajivunia kuwakilisha Ubalozi wa India nchini Tanzania kupitia mbio za riadha ninafikiri tutaacha alama kwa wenyeji,” alisema Soman.

Leave A Reply