The House of Favourite Newspapers

Undani Mchungaji Aliyemfumania Mkewe Kisha Kujiua!

MAMBO mengi mno yanazungu-mzwa juu ya simanzi kuu iliyotawala katika familia ya mchungaji maarufu jijini Harare nchini Zimbabwe, Berry Dambaza aliyedaiwa kujiua baada ya kumfumania mkewe na ‘kibenteni’, Ijumaa lina undani wa mkasa huu.

 

Mchungaji huyo ambaye ni Kiongozi Mkuu wa Kanisa la Kilokole la Upper Room Ministries la nchini Zimbabwe, anadaiwa kujiua kwa kujirusha kutoka ghorofa ya nne kwa kushindwa kuhimili mshtuko wa kumfumania mkewe.

 

POLISI WATHIBITISHA

Mapema wiki hii, polisi wa jijini Harare walithibitisha kifo cha Mchungaji Dambaza, mara tu baada ya kufika eneo la tukio ambalo ni Jengo la Mwalimu Nyerere Way Parkade.

Msemaji wa Jeshi la Polisi la Zimbabwe, Kamishna Msaidizi, Paul Nyathi alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba uchunguzi unaendelea kujua kwa nini mchungaji huyo aliamua kuchukua uamuzi huo au kuna watu walihusika kumuua.

 

“Polisi wanachunguza juu ya tukio la mchungaji kujirusha kutoka ghorofa ya nne hadi chini na kufa eneo la tukio,” alisema Nyathi na kuongeza;

“Mpaka sasa bado hatujapata sababu hasa iliyomfanya kujiua.”

 

AKUTWA NA KIKARATASI

Hata hivyo, katika tukio hilo, mchungaji huyo alikutwa na kikaratasi mfukoni akiomba radhi kwa kuiba pesa, lakini haikueleweka pesa gani.

“Nimefanya makosa mengi, nimeiba pesa nyingi,” ilisomeka sehemu ya ujumbe kwenye kikaratasi hicho.

 

MAMA YAKE NAYE

Ripoti nyingine juu ya tukio hilo zilieleza kuwa, baada ya mchungaji huyo kujiua kwa kumfumania mkewe mwenye umri wa miaka 50, pia mama yake naye alikimbizwa katika Hosiptali ya Parirenyatwa Group ambapo alikata roho kutokana na mshtuko wa kifo cha mchungaji huyo.

 

NI AJALI?

Mmoja wa viongozi wa kanisa hilo alinukuliwa akisema kuwa, inawezekana mchungaji Dambaza hakujiua bali ni tukio la ajali.

Kuna madai mengine kuwa, siku chache kabla ya kifo chake, mchungaji Dambaza alipata ajali ya gari almanusura afe.

 

Meneja Uhusiano wa Kampuni ya Maegesho jijini Harare, Francis Mandaza alisema Mchungaji Dambaza alikuwa mmoja wa wateja wao wakubwa ambaye alikuwa akipaki gari lake eneo hilo la Mwalimu Nyerere Parkade.

 

“Nimeshtuka na kushangazwa niliposikia na kugundua ni mchungaji Dambaza ambaye amejiua,” alisema na kuongeza;

“Tukio lilitokea majira ya saa 12:00 jioni na nilisikia kabla ya kujiua alikuwa akizungukazunguka eneo la maegesho huku akizungumza na wafanyakazi wa chini wenye matatizo.”

 

Mmoja wa wachungaji wenzake kwenye Kanisa la Upper Room Ministries, Bishop Manhanga alisema Dambaza alikuwa na umri wa zaidi ya miaka 50 na alishtuka mno kusikia amekufa katika mazingira tata kama hayo.

 

“Tulipaswa kuwa kwenye mkutano mimi na Mchungaji Dambaza, lakini hakuja kikaoni hadi tulipopigiwa simu na kuambiwa amekufa.

“Hatujui kwa nini amejiua, lakini tunajaribu kutafuta ili kujua kiini cha tukio hili,” alisema mchungaji huyo.

Stori: HARARE, ZIMBABWE, Ijumaa

Comments are closed.