The House of Favourite Newspapers

UONGO MKUBWA WANAOTUMIA WANAUME KWENYEMAPENZI

IPO dhana kwamba wanawake wanapenda kudanganywa kwenye uhusiano wa kimapenzi. Dhana hii imefanya wanaume wengi kuamini kwamba ili kumpata mwanamke unayemtaka, hasa katika kipindi cha kuanzisha uhusiano wa kimapenzi, ni lazima udanganye.

Ukizungumza na wanawake wengi ambao wapo kwenye uhusiano wa kimapenzi, watakueleza kwamba waliwahi kudanganywa siku za mwanzo za uhusiano wao. Upo uongo ambao ni wa kawaida na hauna madhara, lakini uongo mwingne ambao ni mkubwa na madhara yake huwa ni makubwa.

Ukifuatilia pia, wanawake wengi wanaolalamika kuteswa na mapenzi, ni kwa sababu walidanganywa au wanaendelea kudanganywa. Wakati kwa wanaume kudanganya umekuwa ni kama mchezo, kwa wanawake kudanganywa husababisha maumivu makali ya mapenzi. Dhana kwamba wanawake hupenda kudanganywa, si ya kweli hata kidogo.

Yafuatayo, ni mambo ambayo wanaume wengi huwadanganya wanawake wanaotaka kuanzisha nao uhusiano.

  1. UMEOA? UNA MPENZI?

Hili ni swali ambalo mwanamke yeyote unapomueleza kuhusu hisia zako, atataka kulijua. Lakini ukweli ni kwamba wanaume wengi sana hudanganya kwenye swali hili.

Hudhani kwamba ukimweleza mwanamke kwamba nimeoa au ninaye mpenzi, ataona kama lengo lako ni kumchezea kwa hiyo hawezi kukukubali. Matokeo yake, wanaume wengi majibu yao huwa ni ‘hapana sijaoa’, ‘hapana sina mpenzi’ hata kama ukweli ni kwamba wameoa na wana wapenzi wengine.

Ili kuepuka maumivu ya baadaye, unashauriwa kutoamini sana majibu utakayopewa kuhusu swali hili, bali fanya uchunguzi mwenyewe.

  1. UNAFANYA KAZI?

Heshima ya mtu ni kazi! Kwa bahati mbaya, siku hizi ajira zimekuwa ngumu sana kupatikana kwa hiyo kuna kundi kubwa la watu ambao wanaishi bila kuwa na kazi maalum.

Inapotokea umemuuliza swali hili mwanaume, kwa sababu anajua ili aheshimike lazima awe na kazi, hata kama hana kazi atakudanganya. Ni rahisi mwanaume kukudanganya kwamba anafanya kazi kwenye kampuni fulani kubwa, au kwenye ofisi au taasisi kubwa mjini.

Lengo lake anataka kukuhakikishia kwamba yeye ni mtafutaji na utakapokuwa naye, huwezi kupata shida ndogondogo.

Yupo radhi hata kuazima nguo ili aonekane ni wa kishua, ukiingia kichwakichwa umeumia. Wengine hudanganya kwamba wao ni wafanyabiashara wakubwa na kadhalika. Unashauriwa kutoamini majibu ya swali hili mpaka upate ushahidi.

  1. UNA MALENGO GANI NA MIMI?

Wanawake wengi hupenda kabla ya kuanzisha uhusiano, ajue una malengo gani na yeye. Wengi hutegemea kusikia majibu kama nataka tuanzishe familia, nataka nikuoe, nataka nikajitambulishe kwenu na kadhalika na hiyo imefanya wanaume kujifunza namna ya kudanganya.

Unapomuuliza mwanaume swali hili, tegemea kusikia kile kitakachokufurahisha. Atakujibu kwamba atakuoa, atakujibu kwamba anataka uwe wake wa milele na maneno mengine matamu, lakini kumbe anachokitaka ni kutimiza haja zake tu.

Itaendelea wiki ijayo. Kwa maoni, ushauri nicheki kwa namba za hapo juu.

Comments are closed.