The House of Favourite Newspapers

USICHUKULIE POA, MAMBO HAYA MADOGO HUBORESHAPENZI

MARAFIKI ni wakati wetu tena kuzungumza kuhusu uhusiano. Hebu nianze kwa kukuuliza swali, katika kuboresha penzi lako, huwa unafanya nini? Au unadhani ufanye nini ili kuboresha penzi lako?

Hifandhi jibu lako, lakini wengi hufikiria mambo makubwa. Wapo wanaofikiri kuwa kuwanunulia wenzi wao vitu vya thamani kubwa kama cheni ya dhahabu, gari nk ndivyo vyenye thamani pekee!

Si kweli. Ukweli unabaki kuwa, wakati mwingine unaweza kuwa unatamani kumfanya mwenzi wako awe na furaha muda wote lakini mfuko wako ukawa hauruhusu!

Hulka ya wanawake wengi ni kutamani kuona mwenzi wake anamuona wa muhimu na anakuwa naye karibu muda wote. Wanawake hawajali sana vitu vya thamani kama wanaume wanavyofikiri.

 

Kumkumbatia mwanamke na kumbusu katikati ya midomo yake, ukisindikiza na maneno matamu ni zaidi ya gari utakalomnunulia – kikubwa hapa, mwanamke huyo awe kweli ana upendo nawe na si kuwa yupo kibiashara!

Katika mada hii, nimekuandalia vitu vichache ambavyo kwa hakika, kwa mujibu wa utafiti nilioufanya huwapagawisha wanawake. Ukifanya vyote au sehemu yake, unamfanya girlfriend wako ajihisi yupo katika mikono salama.

Bado thamani ya mali na vitu vingine vitabaki katika uhalisia wake, lakini kwa hakika mambo yafuatayo hapa chini, huwachanganya sana wanawake.

 

KADI

Ni utaratibu uliozoeleka sana kipindi cha nyuma kidogo. Sasa hivi teknolojia imeongezeka, kadi inaweza kupatikana hata kwenye mitandao mbalimbali ya internet. Hata hivyo, bado inaonekana kuwa mwanamke anapenda na anatamani kuona mwanaume wake anamkumbuka kwa kumtumia kadi.

Wanaume wengi ni wavivu, lakini kwa sababu ya ustawi wa penzi lako, jaribu hili. Nunua kadi yako yenye ujumbe mzuri, andika maneno mengine kwa mkono wako mwenyewe, pulizia manukato unayotumia, kisha mtumie / mpelekee mpenzi wako. Utakuwa umemroga!

 

NYIMBO, MASHAIRI

Wanawake wanapenda sana kufahamu kuwa kweli alipo anapendwa. Nyimbo nzuri za mapenzi ambazo zitaeleza uzuri wake na namna unavyompenda na kumthamini, vinazidi kukuweka katika kilele cha umiliki uliotukuka.

Mchagulie mpenzi wako wimbo mzuri, kisha mtumie mashairi yake. Au unaweza kuamua kumnunulia rekodi nzuri yenye nyimbo zenye ujumbe mwanana wa mapenzi, utakua umemchanganya sana kwa hakika.

Anachojali mwanamke ni ile hali ya kuona unampenda na unaweza kuthibitisha hilo hata kwa kutumia nyimbo au mashairi mbalimbali ya mapenzi.

Tatizo wanaume wengi hawatilii maanani haya mambo lakini kama unataka kuwa dume la mbegu kwa mwanamke wako, jaribu uchawi huu.

 

LOVE MESSAGES

Kumtumia mpenzi wako ujumbe wa mahaba ni sehemu ya kumwongezea ‘uchizi’ katika penzi lenu. Wengi hawapendi na pengine hawawezi kutunga. Siku hizi mambo ni rahisi sana, magazeti mengi yanaandika Love Messages.

Achana na magazeti hata baadhi ya kampuni za simu hufanya hivyo. Kopi kisha pesti – mtumie. Utaona atakavyozidi kukupaisha kithamani katika maisha yake.

Mfano gazeti dada la hili, Risasi Mchanganyiko linalotoka kila Jumatano kuna safu yenye Love Messages. Unaweza kulitumia ili kumfurahisha mpenzi wako.

 

MITANDAO YA KIJAMII

Siku hizi kuna mitandao mingi ya kijamii. Kwa bahati mbaya, baadhi ya watu huitumia vibaya na kuanzisha uhusiano usiofaa huko. Wanawake wengi huwa hawana amani na wanaume zao hata kama kwenye maelezo yao ya utambulisho wameandika wameoa au wana wachumba.

Kuweka picha yake mara chache au maneno ya kuonyesha unavyompenda, huziba hisia zake mbaya na kujiona yuko na mwanaume huru na makini. Jaribu utaona ukweli wa ninachokisema.

 

KUWA HURU NAYE

Wanaume wengi hawapendi mahaba, lakini asikudanganye mtu, kuongozana na mwenzi wako, huongeza msisimko na kumfanya azidi kuwa huru na mwenye kujiamini. Usimwogope, mshike mkono, tembeeni huku mnamzungumza.

Kichwani hujiona mwanamke kamili, aliye na mwanaume asiye na vimeo mitaani. Haya ni machache kati ya mengi ambayo kwa hakika hustawisha penzi.

Joseph Shaluwa ni Mshauri wa Uhusiano anayeandikia Magazeti ya Global Publishers. Ameandika vitabu vingi, vikiwemo True Love, Let’s Talk About Love na Maisha ya Ndoa vinavyopatikana kwa oda. Kwa sasa anaandaa kitabu chake kipya cha SIRI ZA NDOA YENYE FURAHA kitakachotoka hivi karibuni.

Comments are closed.