The House of Favourite Newspapers

UTAJUAJE KAMA ULIYENAYE NI MTU SAHIHI KWAKO ?

UNAPOANZISHA uhusiano mpya, bila shaka unakuwa na matarajio makubwa ndani ya moyo wako kuhusu yale unayotarajia mwenzi wako atakufanyia au atakuonesha. Hata hivyo, mara nyingi watu wengi husukumwa zaidi na matarajio yao bila kuzingatia kama aliyenaye ni mtu sahihi au la.

Unapojenga matarajio makubwa halafu ukakikosa kile ulichokitarajia, maumivu yake huwa makali sana na wengi hujikuta wakiingia kwenye migogoro mikubwa ya kimapenzi, kwa sababu yale waliyoyatarajia hayajatimizwa na wamejikuta katika mikono isiyo salama. Unapoingia kwenye uhusiano wa kimapenzi, unatakiwa uwe unamjua vizuri mtu uliyemkabidhi moyo wako, lazima uwe na uhakika kama huyo ni mtu sahihi kwako na siyo kusukumwa na sifa za nje au matamanio yako.

Jambo la kwanza ambalo unatakiwa kuwa na uhakika nalo kabla ya kuanzisha uhusiano na mtu, awe mwanaume au mwanamke, ni upendo. Unapoamua kuingia kwenye uhusiano wa kimapenzi, unatarajia mwenzi wako atakupenda kuanzia siku ya kwanza na ataendelea kukupenda kwa dhati kwa sababu hilo ndilo hitaji lako la kwanza katika uhusiano wowote wa kimapenzi.

Ni makosa kuingia kwenye uhusiano ambao unajua wazi kwamba hupendwi ila unaamua tu ‘kujilipua’, sasa kama unajua wazi kwamba hakupendi kuanzia siku ya kwanza utategemeaje atakuja kukupenda mbele ya safari?

Utajuaje kama anakupenda kwa dhati na siyo anakuektia? Maana siku hizi kuna mafundi wa kucheza na mioyo ya watu, atajifanya anakupenda sana lakini kumbe anachokitaka kwako ni kukidhi haja zake au anahitaji msaada fulani kutoka kwako.

Mara nyingi, upendo wa dhati huonekana baada ya muda fulani kupita. Huwezikukutana na mtu leo, kesho mkaanzisha uhusiano halafu ukawa na uhakika kwamba anakupenda, utahitaji muda wa kumchunguza kwa kina, utahitaji kujua anawaza nini kuhusu wewe na anakupa thamani gani maishani mwake.

Lakini pia, matendo ya mtu anayekupenda anapokuwa na wewe huwa hayajifichi, hata kama ataona aibu mkiwa mbele za watu, mkiwa wawili hatashindwa kukushika mkono, kukukumbatia, kukubusu au kufanya kitu chochote kitakachokufanya ujihisi kuwa wa kipekee.

Jambo lingine la muhimu ambalo mtu anayekupenda kwa dhati atakuonesha, ni huruma. Mtu anayekupenda, anaumizwa sana akikuona huna furaha, anaumia sana unapopatwa na jambo baya na muda wote anatamani awepo pembeni yako kukupa msaada.

Lakini mtu asiyekupenda, wala hawezi kuwa anazijali hisia zako, anaweza kukuacha ukiwa unateseka na jambo ambalo lipo ndani ya uwezo wake, yeye akaendelea na hamsini zake, bila kujali chochote. Mtu anayekupenda kwa dhati, pia lazima atakuonesha heshima. Unajua watu wengine ukiwaambia heshima, anaamini kwamba kumsalimu mwenzi wake au kumpigia magoti ndiyo heshima, HAPANA.

Heshima katika mapenzi ina maana kubwa sana na huwa inaanza kwa mtu kuwa anakusikiliza. Ukiona unazungumza naye lakini hata hakusikilizi na yeye anazungumza, mnakuwa mnashindana hata kwa vitu visivyo na msingi, unapaswa kuwa na walakini.

Itaendelea wiki ijayo.

Comments are closed.