The House of Favourite Newspapers

Utaratibu na Sifa za Kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT)

0
Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).

 

Nchini Tanzania kuna aina mblimbali za majeshi ambayo yanafanya kazi tofauti lakini lengo kubwa likiwa ni kuhakikisha kuwa nchi inakuwa salama na yenye amani na utulivu.

Kwa upande wa Jeshi la Kujenga Taifa, limekuwa chimbuko la kuandaa vijana kuajiriwa na vyombo vya Ulinzi na Usalama nchini kama Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza, Usalama wa Taifa na taasisi binafsi za ulinzi.

Jeshi la Kujenga Taifa limekuwa likichukua vijana wa kujitolea na mujibu wa sheria kujiunga katika kambi mbalimbali zilizopo nchini kote.

 

Kuhusu utaratibu wa kujiunga JKT

JKT huandikisha vijana wa kujitolea kutoka mikoa yote ya hapa nchini kila mwaka. Utaratibu unaotumika ni kwa JKT kuandika barua kwa wakuu wa Mikoa na kuanisha nafasi ambazo mkoa umetengewa.

Baada ya Mkoa kupata barua kutoka kwa Mkuu wa JKT na idadi ya nafasi za vijana waliopangiwa kujiunga. Mkoa hugawa nafasi hizo kulingana na wilaya zake. Pia wilaya zinatakiwa kupeleka katika tarafa, kata na vijiji. Mara nyingi uongozi wa wilaya hubandika tangazo la nafasi hizo katika ubao wao wa matangazo.

 

JKT hutangaza nafasi za kujiunga na jeshi hilo kupitia vyombo vya habari vya Serikali na binafsi kwa nia ya kuharakisha taarifa kuwafikia wananchi hasa vijana.

Usaili wa awali hufanyika chini ya Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya wanakotoka vijana hao, baadae hufanyika mkoani, ili kupata idadi ya vijana wa mkoa mzima.

Zoezi hilo linapokamilika mikoani, JKT hutuma timu za maafisa na askari kutoka Makao Makuu ya JKT kwa ajili ya kuhakiki vijana waliosailiwa katika mikoa yote ya Tanzania Bara. Vijana hupimwa afya zao na kusafirishwa katika vikosi vya JKT.

Kwa upande wa vijana wanaotaka kujiunga na JKT kwa njia ya kujitolea, kuna vigezo 7 ambavyo wanatakiwa kutimiza ili kuweza kusajiliwa katika kambi kuanza kupata mafunzo. Vigezo hivyo ni;

1. Awe raia wa Tanzania

2.Awe na Umri kati ya miaka 18-23

3.Awe amemaliza darasa la saba na kuendelea

4.Asiwe ameoa au kuolewa na asiwe na mtu yeyote anayemtegemea

5.Awe tayari kufuata sheria zote za kijeshi zitazokuwa juu yake wakati akiwa jeshini (kutoroka, wizi, ulevi, uvutaji bangi, madawa ya kulevya na upatikanaji wa mimba n.k). Jeshini hayo ni makosa makubwa na utaweza kushtakiwa na kufutiwa mkataba na JKT

6.Awe tayari kurudi nyumbani baada ya kumaliza mkataba wake na Jeshi la Kujenga Taifa

7.Awe na tabia na mwenendo mzuri

Masharti ya vijana wa mujibu wa sheria kwa ajili ya kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa

1.Awe raia wa Tanzania

2.Awe na Umri kati ya miaka 18-35

3.Awe amemaliza kidato cha sita na kuendelea

4.Awe tayari kufuata sheria zote za kijeshi zitazokuwa juu yake wakati akiwa jeshini(Uvutaji bangi, madawa ya kulevya na upatikanaji wa mimba atashitakiwa na kufutiwa mkataba na JKT

5.Utoro haukubaliki na kosa la utoro mkataba utasogezwa mbele

6.Awe na tabia na mwenendo mzuri

Leave A Reply