The House of Favourite Newspapers

Vengu asakwa kwa saa 72

0

Vengu3Mchekeshaji maarufu Bongo, Joseph Shamba ‘Vengu’.

DAR ES SALAAM: Baada ya wasomaji mbalimbali kuonesha hamu ya kutaka kujua hali ya mchekeshaji maarufu Bongo, Joseph Shamba ‘Vengu’, Amani lililazimika kuingia ‘front’ kumsaka msanii huyo kwa takriban saa 72 na kuibuka na majibu yanayokinzana.

MSOMAJI AANZA KUMUULIZIA
Awali, mmoja wa wasomaji wetu aliyejitambulisha kwa jina la Anna Michael, alipiga simu katika chumba cha habari na kueleza kiu aliyonayo kutaka kujua hali ya msanii huyo aliyekuwa akitikingisha alipokuwa na wenzake wa Kundi la Orijino Komedi, Emmanuel Mgaya ‘Masanja Mkandamizaji’, Lucas Mhuvile ‘Joti’, Mujuni Silvery ‘Mpoki’, Isaya Mwakilasa ‘Wakuvanga’ na Alex Chalamila ‘Mac-Reagan’.

“Jamani Global (Global Publishers Ltd; wachapishaji wa magazeti ya Ijumaa Wikienda, Uwazi, Risasi, Amani, Ijumaa na Championi) mbona hamtuletei habari za mchekeshaji Vengu? Yupo wapi siku hizi? Bado anaumwa au ameshapona? Tunatamani kumuona akiwa kwenye runinga.
“Tunamisi vile vituko vyake. Tangu mlipokuwa mnaripoti habari zake za ugonjwa ni miaka kama mitano sasa imepita, hebu fuatilieni mtujuze maana ninyi ndiyo tunawategemea kama chombo cha habari,” alisema.

IMG_1908Mapaparazi wakiwa katika doria jirani na kwa Vengu.

WASOMAJI WENGINE
Kama hiyo haitoshi, kwa nyakati tofauti, wasomaji mbalimbali wamekuwa wakiwauliza wahariri wa magazeti ya Global ambapo wengi wao wamekuwa wakitaka kumjulia hali.

AMANI MZIGONI
Kama ilivyo desturi ya Global kuhakikisha inakata kiu ya wasomaji wake kwa habari za uhakika, liliingia mzigoni ambapo lilifanikiwa kuzungumza na mtu wa karibu na familia (hakutaka jina lake lichorwe gazetini) ambaye alisema amesikia Vengu hajambo na yupo kwenye nyumba yake, Kigamboni-Kibada, Dar.

“Nasikia anaendelea vizuri. Anapiga misele ya hapa na pale. Yupo Kibada kwenye zile nyumba walizokopeshwa na NSSF,” alisema mtu huyo wa karibu na familia.

AMANI LATUA KIBADA
Machi 30, mwaka huu, mapaparazi wa gazeti hili walifunga safari hadi Kibada ambapo walilazimika ‘kupatroo’ kutwa nzima maeneo yanayoizunguka nyumba ya Vengu ili kujiridhisha.
Hata hivyo, jitihada za kumnasa Vengu akipiga misele hazikuzaa matunda kwani licha mapaparazi kutega kamera, hawakufanikiwa kumnasa.

IMG_1931…..Wakiongea na mama wa Vengu.

MAPAPARAZI WABISHA HODI
Mapaparazi walilazimika kubisha hodi katika mlango wa mbele wa nyumba hiyo ambapo waliitikiwa na mwanamke aliyejitambulisha kuwa ni mama yake mdogo Vengu. Alikuwa amekaa kwenye varanda la uani.

Amani: “Mama habari za hapa na mnaendeleaje na hali?”
Mama: “Nzuri tu, za kwenu?”
Amani: “Hatujambo mama, sisi ni waandishi wa habari tumetokea…(mama anakatisha mazungumzo ya mapaparazi).”

Mama: “Aliyewaelekeza hapa ni nani?”
Amani: “Kuna mtu wa bodaboda tumekutana naye (kujaribu kumuondoa wasiwasi) ndiyo tukamuuliza. Tunaona umefanana na Vengu, bila shaka wewe  ni mama Vengu mwenyewe, si ndiyo?”
Mama: “Mimi siyo mama yake mzazi. Mimi ni mama yake mdogo.”
Amani: “Labda utuambie Vengu anaendeleaje?”
Mama: “Hajambo.”
Mapaparazi: “Sijui yupo ndani na tunaweza kumuona au…(mama akatisha mazungumzo).”
Mama: “Hayupo hapa, yupo kwa kaka yake Kunduchi. Halafu ninyi nawajua vizuri, hapa mnanirekodi. Najua sauti yangu mnayo mnataka mkaitumie. Kama mnataka kumuona nendeni Kunduchi kwa kaka’ke?”

IMG_1944….Wakiondoka nyumbani kwa Vengu.

Amani: “Mashabiki wake wametuuliza, wanataka kujua anaendeleaje ndiyo maana tumekuja kuuliza na pengine wanaweza kumpa msaada kama anahitaji.”
Mama: “Hamna lolote. Mlikuwa mnaandika ili muuze magazeti. Wenye lengo la kumsaidia wanaendelea kimyakimya sasa ninyi mnaojifanya kutangaza, hamna lolote.”
Amani: “Basi mama hamna tabu, tunashukuru ngoja twende huko Kunduchi. Si ni kwa yule kaka yake ambaye ni refa (Andrew Shamba) wa mpira wa miguu?
Mama: “Ee huyohuyo.”

KAKA MWINGINE APATIKANA
Wakati mapaparazi wakiendelea kuchimba, waliipata namba ya simu ya kaka mwingine wa Vengu anayefahamika kwa jina la Donat Shamba ambaye alipoulizwa kuhusu hali ya Vengu, hakutoa ushirikiano wa kutosha zaidi ya kusema kama kuna kitu Amani limekipata kuhusu afya ya Vengu liandike.
“Kwanza nani amewapa namba yangu? Sikia nyinyi mmekuwa mkiandika habari nyingi za uongo huko nyuma sisi tulikaa kimya. Sasa naona mnaleta mpya hapa, muulizeni Imelda (mwandishi wa Global ambaye aliwahi kumfokea)… sasa ninyi kama mna ushahidi na mnachotaka kuandika andikeni, mimi sitaki kuzungumzia chochote.”

AMANI LATUA KUNDUCHI
Kwa kuwa siku hiyo muda ulikuwa si rafiki, Machi 31, mapaparazi wetu walifika Kunduchi na kumuulizia refa huyo wakiamini kuwa ni maarufu hivyo ni rahisi kumfikia lakini bahati mbaya kila aliyeulizwa na Amani, alisema hamfahamu.

Kama hiyo haitoshi, Amani lilishinda siku nzima maeneo ya Kunduchi bila mafanikio ambapo jioni mapaparazi walipata wazo la kutafuta namba ya simu ya refa. Akapigiwa simu na alipopokea, alisema yeye haishi Kunduchi na hajawahi kuishi huko hata siku moja.
“Mimi siishi Kunduchi bwana. Naishi Kigogo Freshi, Pugu Kajiungeni. Yaani ukifika tu Pugu Kajiungeni pale mwisho, ukiuliza Kigogo Freshi ukifika tu hapo, ukiuliza hata mtoto mdogo kwa refa ni wapi atakuelekeza. Sema tu leo niko safarini nakwenda Mbeya kuchezesha mechi ya Mbeya City na Coastal Union,” alisema kaka huyo hivyo kulifanya Amani libaini kuwa, Vengu ana kaka wawili tofauti waliotajwa na mama mdogo.

NDANI YA KIGOGO FRESHI SASA!
Kutokana na muda kuwa si rafiki, Aprili  Mosi, mapaparazi wetu walifika Pugu Kajiungeni na kuelekezwa eneo maarufu la Kigogo Freshi ambapo kabla ya kufika kwenye nyumba ya refa, Amani lilizungumza na mmoja wa majirani ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini, akasema Vengu haishi hapo.

MAJIBU TOFAUTI
“Mh! Vengu kama kuishi hapa labda awe amehamia jana usiku lakini siku zote hapa kwa refa najua anaishi yeye, mdogo wa mke wake na mke wake. Tena mkewe leo hayupo. Ameenda kazini. Nafikiri atakuwepo mdogo wake tu ndani, jaribuni kugonga, refa atakuwa kawapoteza maboya bwana, Vengu angekuwepo hapa sisi majirani zake tungejua,” alisema jirani huyo.

NDANI KIMYA
Hata hivyo, Amani lilibisha hodi nyumbani hapo lakini hakukuwa na majibu. Hadi siku hiyo ambayo Amani lilitimiza siku tatu (saa 72) tangu mapaparazi wake wamfungie kazi Vengu, lilibaini kuwa ndugu wa Vengu hususan ‘mama mdogo’ na refa hawakuwa wawazi!

TUJIKUMBUSHE
Vengu aliugua mwaka 2009. Agosti 2011 alizidiwa  ambapo alilazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) jijini Dar. Rais wa awamu ya nne, Jakaya Mrisho Kikwete alikwenda kumjulia hali akiwa hospitalini hapo.
Baada ya hali yake kutotengemaa, alipelekwa kwenye Hospitali ya Apollo nchini India ambako alipatiwa matibabu na kurejeshwa nchini akiendelea kuuguzwa na familia.

Leave A Reply