The House of Favourite Newspapers

VIDEO: Kauli ya Kamanda Sirro Kuhusu Askari Aliyefyatua Risasi Angani

0

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam Kamishna Simon Sirro, leo amezungumza na waandishi wa habari akieleza juu ya mzozo uliotokea baina ya aliyewahi kuwa waziri katika serikali ya awamu ya nne, Adam Malima na Polisi katika eneo la Masaki lililopelekea askari huyo kufyatua risasi kadhaa hewani.

Kamishna Sirro alieleza kuwa Mheshimiwa Adam Malima alikuwa ameegesha gari lake eneo ambalo haliruhusiwi kwa ajili ya maegesho ndipo alipokuja mfanyakazi wa kampuni ambayo ni wakala wa ukusanyaji wa madeni, kukamata teksi bubu pamoja na magari yaliyoegeshwa vibaya akiamuru gari la Malima lipelekwe “yard” ya kampuni hiyo.

Lakini dereva wa Malima likataa na akaamua kuondoa gari katika eneo lilipokuwa limeegeshwa, ndipo askari wa Polisi alipoingilia tukio lile.

“Yule dereva bado alikataa kupeleka gari yard, matokeo yake akaliondoa lile gari na askari wetu alipoona analiondoa lile gari akalirukia na kuingia kwa nguvu kisha akamlazimisha dereva kulirudisha gari lilipokuwa,” alisema kamishna Sirro.

Kamanda Sirro alieleza kuwa wakati mzozo huo baina ya askari na dereva, ndipo alipotokea Malima na kutaka kujua kinachoendelea.

Mfanyakazi anayehusika na ukamataji wa magari yaliyoegeshwa vibaya alimueleza Mh. Malima kuwa gari lake linatakiwa kupelekwa yard kwa kuwa limepatikana likiwa limeegeshwa sehemu isiyoruhusiwa na Mhe. alikataa.

Kuhusu risasi tatu zilizopigwa hewani na askari huyo, Kamishna Sirro alieleza kuwa polisi walikuwa tayari kuondoka katika eneo la tukio, ila kutokana na wingi wa watu na mzozo uliokuwepo pale basi walirudi kwa ujasiri ili kuhakikisha usalama wa eneo lile.

“Kwa hiyo walirudi kwa ujasiri na kwa sababu wale walikuwa wanazomea na mazingira yalikuwa ni hatarishi, hivyo askari wetu ili kuhakikisha anafanikisha ule ukamataji ndipo alipopiga zile risasi tatu hewani, watu wakatawanyika na akamuamuru dereva na Mh Malima kuhakikisha gari hilo linakwenda kipolisi. Dereva na Mh Malima wote wakapelekwa Polisi”

“Kwahiyo utumiaji wa ile silaha ulikuwa  ni kwa ajili ya mazingira yaliyokuwepo na kukubwa zaidi ni ili kusaidia zoezi la ukamataji….” alisema Kamishna Sirro.

Aidha Kamishna Sirro aliwataka wananchi kutambua kuwa suala la utii wa sheria bila shuruti ni la msingi na ukikataa kutii utakamatwa na kupelekwa panapohusika.

Hata hivyo leo, Mh Malima na dereva ambao ni watuhumiwa wamepelekwa Mahakamani leo na kusomewa shtaka linalowakabili la kuzuia Polisi kufanya kazi yao.

VIDEO: Kauli ya Sirro Kuhusu Askari Aliyefyatua Risasi Angani

Leave A Reply