The House of Favourite Newspapers

Vinara Matokeo Kidato cha Sita Baobab Wamkuna Mwalimu Wao

0
Wanafunzi wa shule ya sekondari Baobab ya Mapinga Bagamoyo wakifurahia na mwalimu wao wa taaluma, Edward Logiru baada ya shule yao kufanya vizuri kwenye matokeo ya kidato cha sita yaliyotangazwa na Baraza la Taifa la Mitihani (NECTA) na wanafunzi wawili wa shule hiyo Godwinner Joseph na Vailet Kahyoza kufanikiwa kuingia 10 bora kitaifa.
Wanafunzi wa kiume wa shule ya Baobab ya Mapinga Bagamoyo wakiwa na baadhi ya walimu wao mara baada ya kutangazwa kwa matokeo ya kidato cha sita ambapo wanafunzi wawili wa shule hiyo wamefanikiwa kuingia kwenye 1o bora kitaifa ambapo wanafunzi 62 wa shule hiyo wamefaulu kwa daraja la kwanza, wanafunzi 163 daraja la pili, wanafunzi 108 daraja la tatu na wanafunzi wanne wamepata daraja la nne.

Mwalimu wa taaluma wa shule ya sekondari ya Baobab ya Mapinga Bagamoyo ambayo ni mchanganyiko wa wanafunzi wa kike na wa kiume, Edward Logiru akiwafafanulia matokeo ya kidato cha sita wanafunzi wa shule hiyo ambayo imefanikiwa kuingiza wanafunzi wawili kwenye 10 bora kitaifa kwenye matokeo yaliyotangazwa na NECTA hivi karibuni ambapo ambapo wanafunzi 62 wa shule hiyo wamefaulu kwa daraja la kwanza, wanafunzi 163 daraja la pili, wanafunzi 108 daraja la tatu na wanafunzi wanne wamepata daraja la nne.

 

SHULE ya Sekondari Baobab ya Mapinga Bagamoyo imefanikiwa kufaulisha wanafunzi wote kwenda vyuo vikuu mbalimbali ndani na kufanikiwa kutoa wanafunzi wawili walioingia 10 bora kitaifa.

Pia wanafunzi wote 337 waliofanya mtihani wa kidato cha sita mwaka huu wamefaulu na kupata sifa za kujiunga na vyuo vikuu mbalimbali ndani na nje ya nchi.

 

Akizungumza, Mkuu wa shule hiyo, Venance Hongoa aliwataja wanafunzi walioingia kuwa ni Vailet Kahyoza ambaye amekuwa watatu kwenye 10 bora kitaifa na kwa upande wa wasichana ameshika nafasi hiyo ya tatu.

 

Alimtaja mwingine kuwa ni Godwinner Joseph ambaye amefanikiwa kuingia kwenye kumi bora kitaifa kwa kushika nafasi ya sita na upande wa wasichana kumi bora amekuwa wa tano.

Alisema kwenye matokeo hayo wanafunzi 62 wa shule hiyo wamefaulu kwa daraja la kwanza, wanafunzi 163 daraja la pili, wanafunzi 108 daraja la tatu na wanafunzi wanne wamepata daraja la nne na hakuna hata mmoja aliyeanguka kwenye matokeo hayo.

 

Alitaja siri ya kufaulisha idadi kubwa ya wanafunzi kuwa ni bidii ya walimu ambao wamekuwa wakijituma usiku na mchana kuhakikisha wanafunzi wote wanajiandaa vyema kwaajili ya mitihani ya ndani na ile ya kitaifa.

“Siku zote sisi tunachukua wanafunzi wenye ufaulu wa kawaida sana na hao wengi tuliochukua ni wale waliofanya usaili na wakakosa nafasi shule zingine sisi tukawachukua na kuwatengeneza na sasa wamefaulu vizuri sana tunajivunia kwa hilo,” alisema .

 

Alisema wanafunzi wengi walioingia kidato cha tano waliingia na wastani wa daraja la tatu lakini wamemaliza kwa kupata daraja la kwanza na la pili kwenye matokeo ya kidato cha sita mwaka huu na wazazi wamefurahi sana.

 

“Kwa kulinganisha na walivyoingia na matokeo haya ni mafanikio makubwa sana kwetu na kazi kubwa sana imefanyika tunashukuru juhudi za walimu na ushirikiano wa wazazi, uongozi wa shule na wanafunzi wenyewe, uongozi nao umeweka mazingira wezesha ya kujifunza na kufundisha” alisema

 

Alisema hata kwenye matokeo ya kidato cha pili na cha nne wamekuwa wakifaulisha wanafunzi wengi kwa daraja la kwanza na la pili kutokana na jitihada kubwa inayofanywa na walimu na uongozi wa shule hiyo.

 

“Tunamshukuru kipekee Mkurugenzi wa shule na walimu kwa namna wanavyotupa ushirikiano mkubwa kuhakikisha shule yetu inaendelea kuwa juu mwaka hadi mwaka tunawaomba waendelee kutupa ushirikiano kama huo ili Baobab izidi kuwa juu,” alisema

 

Alitaja siri ya mafanikio hayo kuwa ni mazingira bora ya kufundishia yaliyowekwa na uongozi wa shule hiyo kwa walimu na wanafunzi ikiwemo maabara na maktaba za kisasa za shule hiyo.

 

“Huduma bora za chakula, malazi,  na zahanati iliyoko ndani ya shule ni miongoni mwa vichocheo ya mafanikio yetu tumehakikisha afya imara za wanafunzi maana hawahitaji kwenda nje ya shule kwa matibabu wanatubiwa hapahapa,” alisema

Leave A Reply