The House of Favourite Newspapers

Viongozi, wachezaji Simba wajifungia Taifa

0

 

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, viongozi na wachezaji wa Simba, walijifungia kwa dakika 30 kwenye vyumba vya kubadilishia nguo wakiijadili sare ya mabao 2-2 waliyoipata dhidi ya watani wao wa jadi, Yanga.

 

Timu hizo zilivaana Jumamosi iliyopita jioni kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam katika mchezo wa raundi ya kwanza wa Ligi Kuu Bara uliomalizika kwa sare ya mabao 2-2.

 

Katika mchezo huo Simba ndiyo walikuwa wa kwanza kupata mabao kupitia kwa Meddie Kagere kabla ya Deo Kanda kuongeza la pili huku yale ya Yanga yakipachikwa na Mapinduzi Balama pamoja na Issa Mohamed ‘Banka’.

 

Tukio hilo la aina yake lilitokea mara baada ya mchezo huo kumalizika kwa sare, matokeo ambayo hayakutarajiwa na viongozi na mashabiki wengi wa timu hiyo waliojitokeza kwa wingi uwanjani.

 

Championi Jumatatu ambalo lilikuwepo karibu na vyumba hivyo likifuatilia tukio hilo, lilishuhudia viongozi hao wakifika kwenye vyumba hivyo na kufunga mlango na kuanza kufanya kikao na wachezaji wote.

 

Viongozi walifanya kikao hicho kutokana na kukerwa na matokeo hayo ya sare ambao wenyewe walikuwa wanahitaji ushindi wa mabao mengi na siyo sare waliyoipata.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo gazeti hili limezipata, viongozi walisikitishwa na viwango vya wachezaji wao ambavyo walivionyesha katika mchezo huo uliokuwa wa kuvutia na ushindani.

 

“Mara baada ya mchezo huo viongozi walikuja vyumbani kuzungumza na wachezaji na kikubwa walisikika kulaumu viwango vya wachezaji wao.

 

“Walikerwa zaidi na kitendo cha kukubali kuruhusu kusawazisha mabao yote mawili waliyokuwa wanaongoza ndani ya dakika nne ambazo ni 49 na 52,” alisema mtoa taarifa huyo.

WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam

 

Leave A Reply