The House of Favourite Newspapers

Vodacom Tanzania Kugawa Bonasi ya Bil 25 Kwa Wateja Wake Kupitia M-Pesa

0

Wateja wapatao milioni 11 wa Vodacom Tanzania wanaotumia huduma ya M-Pesa kuanzia leo wataanza kupatiwa mgao wa bonasi kutoka kwenye fungu la shilingi bilioni 25 zilizohifadhiwa kwenye akaunti maalumu ya M-Pesa kwenye mabenki mbalimbali nchini.

Mkurugenzi Mkuu wa Vodacom Tanzania, Ian Ferrao alisema, “Mgao wa fedha hizi kwa wateja wetu ni mwendelezo wa kugawa fedha za bonasi ya M-pesa ambao ni utaratibu wetu. Hapo awali tuligawa takriban bilioni 20; awamu hii inayoanza leo tutagawa bilioni 25 na kuanzia sasa tutakuwa tunatoa gawio kila baada ya kipindi cha miezi mitatu” alisema Ferrao.

Ferrao alisema “kiasi cha fedha atakachopata mteja kwenye mgao wa fedha hizi utategemea matumizi yake ya huduma hii katika kufanya miamala mbalimbali ya malipo ikiwemo kutuma fedha. Natoa wito kwa wateja wetu ambao wameacha kutumia kadi zetu za simu wakati waliwahi kutumia huduma hii wajiunganishe tena kwenye mtandao wetu ili fedha za mgao wao zisipotee bure. Pia wateja wetu wanaotumia huduma hii kuanzia leo wanaweza kuangalia fedha watakazojipatia kwa kutuma ujumbe wa maneno kwa kuandika neno KIASI na kuutuma kwenda namba 15300

 

Aliongeza kusema kuwa wateja wa huduma ya M-Pesa wakiwemo mawakala wakubwa na wadogo wanao uhuru wa kutumia fedha zao za mgao watakazopata ambapo wanaweza kuzitumia kununulia huduma mbalimbali za Vodacom kama muda wa maongezi,kujiunga na vipurushi mbalimbali ikiwemo  kifurushi cha DABO BANDO kinachomuwezesha mteja kununua muda wa maongezi na vifurushi vya internet moja kwa moja kwa kutumia M-Pesa, wanaweza kuzituma fedha hizo kwa ndugu na marafiki, kulipia ankra zao mbalimbali au kujiwekea akiba kwenye akaunti za M-Pawa kwenye simu zao. Vodacom pia imetangaza kuwa itaendelea kuboresha huduma za M-Pesa ili utumiaji wake ulete unafuu kwa wateja pia kuwanufaisha mawakala wake.

Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa M-Commerce wa Vodacom Tanzania, Sitoyo Lopokoiyit, amesema kuanzia mwezi uliopita imepunguza viwango vya makato kwa watumiaji wa huduma  ya M-Pesa kwa miamala ya hadi shillingi 40,000 kwa asilimia 40% hali inayoleta unafuu kwa wateja na mawakala kuendelea kujipatia faida ya kutoa huduma “M-Pesa imeleta mapinduzi makubwa ya  huduma za kifedha nchini ikiwa na mtandao wa mawakala zaidi ya 85,000.

Leave A Reply