Wahitimu St Mark’s Waaswa Kutojiingiza Kwenye Utumiaji Dawa za Kulevya
Wazazi na walezi wametakiwa kutokimbilia shule zenye ufaulu kwa ajili ya kuwapeleka watoto wao na kuaswa kuwatafutia shule zitakazowajenga kimaadili ili wasijekujiingiza kwenye utumiaji wa dawa za kulevya.
Akizungumza wakati wa mahafali ya 17 Mkurugenzi Mtendaji wa shule ya St. Mark’s Peter alisema kuwa baadhi ya wazazi, wanakimbilia shule zenye ufaulu lakini wanashindwa kuelewa kuwa kuna shule zinaufaulu lakini haziwajengei watoto maadili.
” Kabla ya kumpeleka mtoto shule mzazi ufuatilie shule hiyo ina maadili au haina na Kama haina usikimbilie sifa za ufaulu pekee na ukampeleka mtoto,” amesema.
Aliongeza kuwa kama mtoto atakuwa hana maadili na akafaulu vizuri mitihani yake lakini anapopata ajira hawezi kufanya kazi vizuri kutokana na kutokuwa na maadili mema.
Aliendelea kwa kusema shule yao imeanzisha sera ya usalama kwa watoto wakiwa ndani ya shule na nje ya shule.
” Tumeanzisha sera yetu tunawalinda watoto na matendo ya usalama nje na ndani ya shule.
“Mtoto akitoa taarifa kuwa nyumbani ananyanyaswa tunafuatilia taarifa hizo ili tuweze kuzishughulikia.
“Naipongeza Serikali ya awamu ya tano kwa kuboresha elimu ambapo kwa sasa watoto wengi wanapata elimu na natoa nasaha kwa wahitimu maadili mliyoyapata hapa mkayandeleze mnapokuwa mitaani,”alisema mkurugenzi huyo.
Aidha amewataka wahitimu hao wasijiingize katika makundi yasiyofaa ikiwemo na kujihusisha na matumizi ya madawa kulevya.