Wanahisa Waongeza Mtaji Mkombozi Commercial Bank, Wateja Waula
Benki ya Mkombozi Commercial inayomilikiwa na Kanisa Katoliki pamoja na wanahisa yenye Makao Makuu Msimbazi Center Jijini Dar, jana Septemba 12 ilifanya mkutano wake wa 11 na wanahisa wake.
Katika mkutano huo wanahisa hao walijadili mambo mbalimbali ikiwemo jinsi ya kuipanua zaidi benki hiyo na kuiongezea mtaji ili kuwanufaisha wateja wao.
Akizungumza na wanahabari baada ya mkutano huo, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa benki hiyo, Profesa Marcelina Chijoriga amesema katika mkutano huo wamekubaliana na wanahisa hao kuongeza mtaji na kufikia bilioni 15 kwa ajili ya maboresho ya benki hiyo.
Profesa Marcelina amesema benki hiyo yenye miaka 11 sasa imeweza kujitanua na kufikia matawi 11 nchi nzima jambo linaloonesha maendeleo ya kasi kulinganisha na benki zingine. Ameendelea kusema kuwa wanahisa hao kwa pamoja wamekubaliana kuitanua benki hiyo na kuanzisha kutoa huduma kupitia mawakala nchi nzima ili kuwafikia wateja wao kiurahisi.
“Tunawashauri wananchi popote walipo waje kujiunga na benki yetu ambayo inatoa huduma kwa gharama nafuu ambapo pia kuna akaunti ya Mwanajuiya ambayo hii haina makato yeyote”.
Akizungumzia mikopo, Profesa Marcelina aliwataka wananchi wote bila kuangalia dini zao wala madhehebu yeyote anaruhusiwa kwenda kukopa kwenye benki hiyo ambayo mikopo ina riba ndogo kabisa. Alimaliza kusema Profesa Marcelina.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Respige Kimati amesema benki hiyo imelenga kujitanua zaidi na kuwafikia wateja sehemu mbalimbali mpaka vijijini ambapo kuna changamoto za huduma za kibenki.
“Pamoja na maboresho makubwa tutakayofanya lengo letu ni kupunguza gharama kwa wateja wetu ili kuwapa unafuu”. Alimaliza kusema Profesa Marcelina.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa benki hiyo, Askofu Beatus Kinyaiya amesema benki nyingi hivi karibuni zilipitia changamoto kufuatia ugonjwa wa Covid-19 unaosababishwa na virusi vya corona na kuyumba kiuchumi kutokana na wateja wao haswa wakopaji kushindwa kurejesha marejesho ya mikopo lakini kwa upande wao amesema mambo yanakwenda vizuri.
Hivyo Askofu huyo amewataka wananchi bila kuangalia dini wala madhehebu yao wafike kwenye benki hiyo kujipatia huduma zao.
HABARI/PICHA:RICHARD BUKOS /GPL