Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ally Salum Hapi akizungumza na wanachama wa CWTF.
WAIGIZAJI wa filamu wanawake nchini wamepongezwa kwa kuunda chama chao cha maendeleo na kuchukua hatua ya kujitolea kuchangia damu kwa wananchi wenzao wanaohihitaji.
Waigizaji hao wakimsikiliza DC Ali Hapi.
Hayo yalisemwa jana na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ally Salum Hapi, wakati akiongea na wasanii hao alipowapongeza kwa kujitolea kuchangia damu katika Hospitali ya Mwananyamala ambapo alikuwa mgeni rasmi pia katika hafla ya kuzindua chama cha wasanii hao cha maendeleo kijulikanancho kama CWTF.
Mkuu huyo wa wilaya aliwapongeza wasanii hao kwa kuamua kuunda chama hicho na kuanza na mpango wa kujitolea damu kwa ajili ya kuokoa maisha ya wananchi wenzao ambapo aliwapa pia fursa ya kuandaa tamasha kubwa zaidi ambalo litawafanya wajitangaze zaidi na kuwasihi kujiamini kwani umoja huo ni jambo jema.
Mwigizaji Blandina Chagula ‘Johari’ akijiburudisha baada ya kuchangia damu.
“Umoja mliouanzisha ni jambo jema, ninawapongeze na kwa kiasi kikubwa naamini mmefanikiwa katika zoezi hili, hivyo nawasihi kutoishia hapo kwani mlichokifanya ni kitu kikubwa na cha mfano hivyo nawahamasisha kuandaa tamasha kubwa zaidi ambalo naamini nitawaunga mkono kuhakikisha mnafanikiwa na hapo ndipo mtajitangaza zaidi, ”alisema Hapi.
Mkuu huyo alisema kuwa wakati wowote anawapa nafasi ya kufika ofisini kwake kwa ajili ya suala lolote la maendeleo kwani anaamini penye msanii kuna maendeleo na kwamba msanii ni kioo cha jamii.
“Pia nawasihi muendelee kujiamini kwa kugombea ngazi mbalimbali za uongozi nchini kwani naamini mnaweza na fursa nyingi zipo,” alisisitiza mkuu huyo aliyelitembelea eneo lililokuwa likifanyiwa utoaji damu salama, hafla iliyoandaliwa chini ya mwenyekiti wao Vanitha Omary.
Mwigizaji Salome Urassa ‘Thea’ akichangia damu.
Miongoni mwa mastaa wa filamu walijitolea damu ni Salome Urassa ‘Thea’, Nahya Stanslaus ‘Nina’, Happiness Stanslaus ‘Nyamayao’, Blandina Chagula ‘Johari’ na Halima Yahya ‘ Davina’ .
Na Hamida Hassan/GPL
Comments are closed.