WATANZANIA wameshuariwa kuwekeza katika masoko ya fedha ili kunufaika na fursa zinazopatikana katika masoko hayo ambayo hayahitaji mtaji mkubwa wa kuanzia imeelezwa.
Ushauri huo umetolewa na Mkurugenzi wa Idara ya Hazina na Masoko wa Benki ya NBC, Peter Nalitolela katika warsha maalumu iliyoandaliwa na NBC kwa wanafunzi wa Shule ya Biashara ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDBS), iliyofanyika chuoni hapo, Dar es Salaam hivi karibuni.
Alisema lengo kubwa la warsha hiyo ni kunoa uelewa wa wanafunzi hao kuhusu masoko ya fedha, ili wawe na uwezo wa kuchangamkia fursa lukuki zilizopo sokoni hapo punde wanapomaliza masomo yao.
“ Kuna kasumba iliyojengeka miongoni mwa watu wenye vipato vya wastani kuwa kuwekeza katika masoko ya fedha ni ghali na ni eneo la uwekezaji ambalo limeachiwa matajiri, kitu ambacho hakina ukweli wowote ukiangalia hali halisi”, alisema mkurugenzi huyo.
Bwana Nalitolela aliongeza kuwa kiwango cha chini kabisa kinachohitajika kuwekeza katika soko la fedha ni shilingi sita, fedha ambayo alisema inaweza kupatikana kwa mtu yeyote aliyejiwekea malengo ya dhati ya kutunza fedha kwa ajili ya kuwekeza kwa manufaa yake ya baadaye.
Nalitolela alisema cha kushangaza, watu wengi ambao wanajichukulia kuwa wenye kipato cha chini wana tabia ya kuwekeza kwenye biashara zilizozoeleka kama kununua daladala au kufungua duka la rejareja, miradi ambayo kiuhalisia inahitaji mtaji mkubwa kupindukia ule unaohitajika kuwekeza katika hati fungati, hisa au dhamana.
“ Tunawashauri watanzania wawekeze kwenye makampuni mengi yaliyobinasishwa na ambayo yanafanya vizuri kibiashara, ili washiriki katika kuendesha uchumi wao na vilevile wajizolee sehemu ya faida inayotengenezwa na makampuni hayo,” alisema Nalitolela.
Aidha kuhusu mafunzo hayo Nalitolela alisema kuwa mafunzo hayo ni sehemu ya mpango wa NBC kutumia sehemu ya faida yake kusaidia ustawi wa jamii, na yanalenga kuwapatia wanafunzi wanaosomea fani za fedha na benki katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam stadi za masoko ya fedha ili kuwaanda kuyatumia na kufaidika nayo.
“ Haja hii ndiyo inaleta msukumo wetu wa kuelemisha wanafunzi ili watambue ni jinsi gani elimu yao ya darasani inahusiana na hali halisi kwenye masoko ya fedha. Kama mtoaji mkongwe wa huduma za fedha, NBC itaendelea kuhamasisha umma ili kupanua wigo wa matumizi ya masoko ya fedha.”
Comments are closed.