VIDEO: 62 Wafariki Ajali ya Lori la Mafuta Moro, 70 Wajeruhiwa
MKUU wa Mkoa wa Morogoro, Dkt. Stephen Kebwe, amesema imepatikana miili ya watu 60 waliokufa kutokana na malipuko wa moto kufuatia lori la mafuta kupinduka eneo la Msamvu mjini Morogoro.
Akizungumza leo, Agosti 10, 2019, Kebwe alisema watu hao ambao miili yao imehifadhiwa katika Hospitali ya Mkoa, wamefariki baada ya kuanza kuchota mafuta kutoka kwenye lori hilo.
Aliongeza pia kwamba watu 70 wamejeruhiwa katika tukio hilo na wanapata matibabu katika hospitali hiyo.
Naye Mganga Mkuu wa hospitali hiyo, Dkt. Ritha Lyamuya, amesema hadi kufikia mchana, walikuwa wamepokea miili 62.
“Majeruhi tuliowapokea hapa ni wanaume 52 na wanawake wanane. Tumelazimika kuwaomba madaktari na wauguzi kutoka hospitali na vituo vingine vya afya katika manispaa ya Morogoro kusaidia katika jukumu hili wa kuwa leo ni mapumziko kwa wengi wao,” amesema Lyamuya.
Akizungumza kuhusu chanzo cha ajali hiyo, Kebwe amesema dereva wa lori alikuwa anamkwepa dereva wa bodaboda na kusababisha lori hilo kupinduka.
“Kwenye lori kulikuwa na watu watatu; dereva, kondakta na mwanamke mmoja. Dereva na huyo mwanamke walikuwa wamebanwa katika lori hiyo ambapo watu walijitahidi kuwaokoa,” amesema Kebwe.
Comments are closed.