The House of Favourite Newspapers

Waziri Kairuki  Azindua  DVD za Nyimbo za Kwaya ya  Gethmane

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Uwekezaji, Angella Kairuki (katikati) akiwa ameshika DVD mbili za Petro na Sikiliza baada ya kuzizindua rasmi katika Ukumbu wa Uhuru jijini Dar es Salaam. DVD hizo ni za kwaya ya Gethmane ya Kanisa la Wasabato Mtaa wa Kinondoni .Kulia ni Mchungaji wa Kanisa hilo Masanya Anthony pamoja na waalikwa wengine wakishuhuhudia uzinduzi huo.
Waziri wa Nchi,Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Uwekezaji Angella Kairuki akishiriki kuimba na kucheza wimbo wa Injili wa Kanisa Sabato wakati wa uzinduzi wa DVD mbili za kwaya ya Gethmane.
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Uwekezaji, Angella Kairuki ameipongeza Kwaya ya Gethmane ya Kanisa Wasaabato Mtaa wa Kinondoni jijini Dar es Salaam kwa kutunga na kuimba nyimbo za Injili zinazozungumzia umuhimu wa Watanzania kuendelea kudumisha  amani,umoja na upendo.
Kairuki ametoa pongezi hizo jijini Dar es Salaam baada ya kuzindua DVD mbili za  Sikiliza na Petro za Kwaya ya Gethmane ambapo kabla ya kuzizindua alipata nafasi ya kusikiliza nyimbo kadhaa na kukoshwa na aina ya ujumbe uliopo katika nyimbo zao.
“Kwa kweli nimefurahishwa na ujumbe ambao uko kwenye nyimbo za kwaya hii.Ni jambo nzuri kuona na kusikia Watanzania tukihamasishana kudumisha amani, umoja na mshikamano.Kwaya ya Gethmane ambayo sasa inatumiza miaka 10 tangu kuanza kwake kwa kutumia nafasi yao wametambua jukumu hilo  na hivyo wametunga nyimbo mahususi kuzungumzia amani ,upendo na mshikamano.
“Hili ni jambo la kupongeza na kutoa rai kwa waimbaji wa nyimbo mbalimbali zikiwemo nyimbo za Injili kuimba nyimbo za kuhamasisha amani na mshikamano. Tunafahamu  Oktoba 14 tunaadhimisha miaka 20 ya kifo cha Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Nyerere.Tunakumbuka alivyosimama imara kusimamia amani na kuwafanya Watanzania kuwa wamoja, ni jukumu letu kumuenzi kwa kukumbusha umuhimu wa kuwa wamoja ,”,amesema Waziri Kairuki.
Waziri Kairuki aliyekuwa mgeni rasmi pamoja na mambo mengine ametumia nafasi hiyo kueleza kuwa kuna kila sababu ya Watanzania  kuendelea kuheshimu uhuru wa kuabudi kwa kila mtu na dini yake au dhehebu lake na hakuna aliyebora zaidi ya mwingine.
Pia Waziri Kairuki ameongeza Serikali inatambua mchango mkubwa unaofanywa na watanzania wa kulinda amani iliyopo na wao kama Serikali wataendelea kuilinda amani hiyo kwa gharama yeyote ile. “Ni jambo la muhimu sana  kila mtu kuheshimu dini ya mwingine,”amesema.
Wakati huo huo Waziri Kairuki ameongeza harambe ya kuchangia kwaya hiyo kwa ajili ya kuendeleza malengo na mipango ya maendeleo na kuitumia jamii kupitia nyimbo za Injili ambapo fedha na ahadi zaidi ya Sh.milioni 25 zimepatikana kutoka kwa waalikwa waliohudhuria uzinduzi wa DVD hizo.
Kwa upande wake Mchungaji wa Kanisa hilo la Wasabato Mtaa wa Kinondoni jijini Dar es Salaam Masanya Anthony ameema kuwa Kanisa wanatambua umuhimu wa nchi ya Tanzania kuendelea kuwa yenye amani na hivyo wataendelea kuliombea Taifa na viongozi wake wakati wote.
“Kanisa letu tunalo jukumu la kuliombea  Taifa na tutaendelea kufanya hivyo siku zote.Waziri Kairuki tunaomba ufikishe salami zetu kwa Rais wetu Dk. John Magufuli na mueleze kuwa Kanisa la Wasabato Kinondoni tunatambua kazi kubwa unavyofanya Rais ya kuijenga nchi yetu. Kwaya yetu pamoja na nyimbo nyingine za injili imeamua kuwa na nyimbo za kuzungumzia amani na kuisifu nchi yetu nzuri,”amesema Mchungaji Anthony.

Comments are closed.