The House of Favourite Newspapers

Waziri Mhagama Azindua MasterCard QR Ya Malipo Kwa Bodaboda Ya NMB

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Jenista Mhagama akizungumza jambo katika hafla hiyo

Benki ya NMB imezindua malipo ya kimtandao kwa huduma za bodaboda.

Mfumo huo wa malipo ni wa aina yake na wa kwanza nchini unaowawezesha abiria na wateja wa bodaboda kulipa nauli zao kwa kutumia simu zao za mkononi na fedha hizo kwenda moja kwa moja kwenye akaunti ya NMB ya dereva husika.

Afisa Mkuu wa Wateja Binafsi, Biashara ndogo na za Kati wa NMB, Filbert Mponzi akizungumza kwenye hafla hiyo.

Huduma hiyo iliyozinduliwa jana ni mwendelezo wa juhudi za kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanatumia huduma za benki sambamba na kuhamasisha utunzaji fedha kwa njia salama na za uhakika.

Akizungumza kwenye uzinduzi wa huduma hiyo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu – Jenista Mhagama alisema huduma hii inaweka msingi wa kurasimisha sekta ndogo ya usafiri wa bodaboda.

“Mnachokifanya leo kina baraka zote za Serikali. Hiki kitawasaidia vijana kuongeza umakini kwenye shughuli zao na kuchangia uchumi wa Taifa,” amesema Mhagama.

Kaimu Mkurugenzi wa NMB, Ruth Zaipuna akizungumza kwenye hafla hiyo.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NMB – Ruth Zaipuna alisema huduma hiyo inatoa fursa kwa maelfu ya madereva wa bodaboda nchini kutumia huduma za benki hatua ambayo itaimarisha usalama wa fedha zao pamoja na wao wenyewe.

“Hii ni namna bora zaidi ya kurudisha uwajibikaji kwa shughuli za madereva wa bodaboda ambao mchango wao kwenye uchumi wa Taifa unatambulika. Tunazindua huduma hii jijini Dar es Salaam kisha tutaenda Mwanza, Arusha, Ruvuma, Dodoma na Mbeya wiki chache zijazo,” amesema Zaipuna.

Mfumo huo wa malipo utawasaidia madereva bodaboda kukuza biashara zao kwa kuwapunguzia adha ya kuhifadhi fedha taslimu na kuwapa fursa ya kuepuka matumizi yasiyokuwa na mpangilio.

“Kwa kutumia MasterCard QR, tunatoa huduma ya uhakika wa malipo kwa madereva bodaboda kutoka kwa watoa huduma wote na benki za biashara wanaotumia huduma hii. Malipo yatafanywa kwa kutumia simu ya mkononi yenye programu ya MasterCard QR na kupunguza hatari za kumiliki fedha taslimu. Huduma hii kwa bodaboda ni sehemu ya mkakati wa benki kufikisha huduma zake kwa watu wengi zaidi,” amesema Zaipuna .

Mwendesha Bodaboda, Masoud Seif akiwa amempakia Waziri, Jenista Mhagama wakati wa uzinduzi wa huduma ya NMB MASTA BODA.

Mwakilishi wa MasterCard Tanzania – Frank Molla amesema mfumo huo wa malipo ya kidijiti unakusudia kuwapa uhuru dereva na abiria wake wakati wote wa safari huku ukimuepushia dereva uwezekano wa kuporwa au kupoteza fedha zake.

“MasterCard inakusudia kuhamasisha na kuwezesha malipo ya kidijiti hapa nchini. Benki ya NMB inayo dira inayofanana nasi katika ujenzi wa miundombinu itakayoiwezesha jamii kufurahia ulimwengu wa malipo ya kimtandao kwa kutumia teknolojia ya kisasa,” amesema.

Tayari Benki ya NMB imewajengea uwezo zaidi ya madereva 1,000 wa jinsi ya kutumia QR kufanikisha malipo kwa kutumia simu za mkononi. Mfumo huo unatarajiwa kuongeza usalama wa malipo ya kimtandao kwa sekta hiyo ndogo ya watoa huduma.

Kumlipa bodaboda, abiria anatakiwa kwenda kwenye simu yako – NMB Mkononi, piga *150*66# kupata menu na kuchagua kufanya malipo halafu ‘Scan to Pay.’ Pia ukiwa na simu janja nenda kwenye programu (App) ya NMB Mkonini ambako atachagua ‘Scan to Pay’ na kuendelea na maelekezo.

Comments are closed.