The House of Favourite Newspapers

Waziri Mkuu Apokea Msaada wa Madawati kutoka Coca-Cola Kwanza

0
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa (kulia) akifurahia jambo na Mkurugenzi wa Mawasiliano Coca-Cola Kwanza Salum Nassor baada ya kampuni hiyo kukabidhi madawati kwa wilaya ya Ruangwa.

 

Kampuni ya vinywaji baridi ya Coca-Cola Kwanza Ltd mwishoni mwa wiki imetoa msaada wa madawati 100 kwa Wilaya ya Ruangwa katika Mkoani wa Lindi, ikiwa na malengo ya kuunga juhudi za serikali katika kuboresha Sekta ya Elimu katika maeneo ya vijijini.

Msaada wa madawati hayo yenye thamani ya Sh10 milioni ulipokelewa na Waziri Mkuu ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Ruangwa Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa na lengo lake kuu ni kuinua sekta ya elimu vijijini pamoja na kutatua changamoto za uhaba wa madawati kwenye shule za msingi na hasa kwa maeneo ya vijijini

Akizungumza wakati wa kukabidhi madawati hayo, Mkurugenzi wa Masuala ya Umma na Mawasiliano Coca-Cola Kwanza, Bwana Salum Nassor alisema mchango wa kampuni hiyo ulilenga kurudisha kwa jamii sehemu ya faida yake.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiwa amekalia moja ya madawati yaliyotolewa na kampuni ya Coca-Cola Kwanza kwa wilayani Ruangwa mkoani Lindi. Kampuni ya Coca-Cola ilitoa madawati 100 yenye thamani ya milioni kumi ikiwa ni moja ya kuunga mkono juhudi za serikali kwenye sekta ya elimu na hasa kwa maeneo ya vijijini. Kushoto ni Mkurugenzi wa masuala ya Umma na Mawasiliano Coca-Cola Kwanza

“Lengo la Coca Cola Kwanza ni kuboresha maisha ya Watanzania katika sekta mbali mbali ikiwamo elimu na hii ni moja ya sababu ya kutoa madawati haya kwa Wilaya ya Ruangwa,” alisema.

 

Nassor ameongeza, “Siku zote tunafanya biashara kwenye jamii ambayo tunaishi nayo kila siku. Kurudisha sehemu ya faida yetu kwa jamii imekuwa ni desturi yetu. Msaada wa madawati haya 100 utasaidia wanafunzi 200 kukaa kwa pamoja ni hivyo kutatua changamoto ya madawati kwa shule husika.

 

Nassor alitoa wito kwa taasisi zingine, wadau, na mashirika yasiyo ya serikali kushirikiana na kuunga mkono juhudi za serikali katika kutafuta suluhisho la baadhi ya changamoto kwenye jamii yetu.

Kwa upande wake, Mbunge wa Ruangwa ambaye pia ni Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa alisema msaada wa madawati kutoka Coca-cola Kwanza unaonyesha uhusiano mzuri uliopo baina ya serikali na sekta binafsi, ambayo inanufaisha jamii.

 

Majaliwa aliongeza; Mchango huu wa madawati kutoka Coca-Cola Kwanza umekuja wakati muafaka wa kuanza mwaka mpya wa masomo ambapo tunashuhudia idadi kubwa ya wanafunzi wanaojindikisha kuanza masomo kutoka na elimu bure inayotolewa na serikali. Kwa sababu hiyo, ni jukumu letu kila mmoja kuhakikisha kuwa madawati haya yanatunzwa vizuri kwa manufaa ya wanafunzi waliopo kwa sasa na hata kwa wale ambao watajiunga na shule kwa siku za usoni.

 

Coca Cola Kwanza ni kampuni tanzu ya  Coca-Cola Afrika kutoka Afrika Kusini ambayo imekuwa na kipaumbele kwenye kutengeneza madawati pamoja na kuyazambaza kwenye maeneo yenye upungufu ikiwa ni juhudi za kuunga mkono serikali kwenye kutoa elimu bure tangu 2017. Mpaka sasa, kampuni ya Coca-Cola Kwanza imeweza kutengeneza na kusambaza madawati zaidi ya 3,100 kwenye shule tofauti hapa nchini.

Leave A Reply