The House of Favourite Newspapers

YAJUE MAZOEA MABAYA KWENYE UHUSIANO

KATIKA zama hizi za Sayansi na Teknolojia, uzungu umekuwa mwingi kwenye uhusiano. Kutokana na hilo, wapenzi hudanganyana kwa kuiga tabia za watu wa Magharibi kwa kufanya mambo yaliyo kinyume na desturi zetu, lakini pia kanuni za afya.

Baadhi ya vijana wamejikuta wakidanganyika na kuingia kwenye mazoea yasiyofaa ambayo baadaye husababisha madhara makubwa. Waliongia kwenye michezo hiyo awali hawakujua kama kuna athari, hivyo kwako wewe ambaye hujaanza, itakusaidia kuelewa kwa kina na hatua za kuchukua.

Twende darasani…

 

KINYUME NA MAUMBILE

Mchezo huu umeingia kwa kasi sana kwenye jamii yetu. Waanzilishi wakuu wa ujinga huu ni wanaume. Kiukweli, baadhi ya wanawake wamejikuta kwenye wakati mgumu kwenye mapenzi baada ya baadhi ya wanaume wa kileo kucharukia kuanza mapenzi kwa njia hii isiyokubalika.

“Kaka Shaluwa, mpenzi wangu ananing’ang’aniza sana nifanye naye huu mchezo, anasema eti amesikia marafiki zake wakisema tukifanya, eti mapenzi yataongezeka! Sijui kama kuna ukweli wowote, hebu niambie kaka yangu,” huyu ni msomaji wangu kutoka Mbeya ambaye aliniomba ushauri kwa njia ya simu.

 

Ipo mifano mingi, lakini yupo dada mmoja aliwasiliana nami, akaniambia kwamba anafanya mchezo huo kwa mwaka wa tatu sasa kwa lengo la kulinda usichana wake. Nilizungumza naye mengi na kumweleza madhara makubwa ambayo anaweza kuyapata kwa kuendekeza mchezo huo.

Kifupi si tabia nzuri kuiendekeza na husababisha madhara makubwa sana kiafya. Ikitokea mpenzi wako ameonyesha kuhitaji mchezo huu, kaa naye mbali. Ni dhahiri hana mapenzi ya dhati kwako.

Unaweza kuanza kwa kumuelimisha athari zake, huenda hazijui ila ukiona anaendelea kukung’ang’aniza, mwache aende!

 

ATHARI ZAKE NI ZIPI?

Zipo athari za moja kwa moja ambazo mhusika anaweza kuzipata. Kwanza inakupasa ujue kwamba, njia hiyo ni maalum kwa ajili ya kupitisha kinyesi tu na siyo kitu kingine chochote.

Mwanamke anaweza kupata magonjwa ya uambukizo ya njia ya haja kubwa. Mafuta mepesi yaliyopo kwenye njia hiyo muda wote kwa lengo la kupitisha kinyesi kirahisi, yatakauka kutokana na matumizi mapya ambayo mhusika atakuwa ameyaanza.

 

Kukauka kwa mafuta hayo husababisha choo kutoka kwa tabu na hatimaye kuacha mikwaruzo ambayo husababisha vidonda – mwisho wake kupata maambukizi ya virusi ambavyo humea siku zote kwenye njia hiyo.

Hii ndiyo sababu mwanamke hushauriwa kutawaza akianzia njia ya haja ndogo kuelekea haja kubwa ili kuepusha maambukizi ya virusi vilivyopo kwenye njia ya haja kubwa. Zaidi ya yote ni vidonda na maumivu makali wakati wa kupata haja kubwa.

Misuli inayodhibiti haja kubwa hulegea na hivyo kuwepo kwa hatari ya kutokwa na haja bila taarifa. Kwa maneno mengine, mfanyaji wa kitendo hicho anajiweka kwenye hatari ya kuanza kutumia nepi akiwa mtu mzima!

 

Zaidi ya yote, wakati wa kujifungua mwanamke hupata tabu kwa sababu hatakuwa na uwezo wa kusukuma mtoto na hivyo kuwepo kwa uwezekano mkubwa wa kujifungua kwa njia ya upasuaji.

Ukiachana na wanawake, wanaume pia wanakuwa kwenye hatari kubwa ya kupata maradhi ya kuambukiza (rejea hapo juu). Kadhalika mwanaume anakuwa kwenye nafasi kubwa ya kupata magonjwa mengine ya njia ya mkojo, kama mrija kuziba na mengineyo ya kitaalam ambayo matibabu yake wakati mwingine huhitajika kufanyika upasuaji.

 

TAFAKARI ZAIDI

Una haja gani ya kuingia kwenye matatizo makubwa kiafya? Una sababu gani ya kuwa kwenye hatari kubwa kiasi hiki? Kimsingi hakuna starehe yoyote ya maana inayopatikana kwa kufanya mapenzi kinyume na maumbile (labda kwa sababu ya mazoea mabaya unaweza kuona tofauti).

Mbaya zaidi, hakuna kitabu chochote kitakatifu kinachounga mkono tabia hii. Imani zote zinakinzana na ufanyaji wa mapenzi kinyume na maumbile.

Hebu ufike wakati sasa wa kuyatazama madhara haya kama somo, ikiwa unafanya mchezo huu, achana nao mara moja maana upo kwenye hatari kubwa.

 

Kama hujawahi, ondoa fikra hizo kabisa kichwani mwako. Ni bora kuachana na mwanaume anayelazimisha mchezo huo kuliko kuwa naye kwa kuogopa kukosa ndoa.

Kwanza ndoa na mtu wa aina hiyo ya kazi gani? Subiri aliye na adabu zake, mwenye kujali utu na heshima yako anakuja. Muda haujawahi kudanganya!

Kwa leo naomba niishie hapa, wiki ijayo tutaendelea, USIKOSE!

Joseph Shaluwa ni Mshauri wa Uhusiano anayeandikia Magazeti ya Global Publishers.

JIUNGE NA FAMILIA YA GLOBAL TV UPANDE MTANDAO WA MAFANIKIO

Bofya hapa kujiunga na familia ya Global TV Club ==> Global TV Family Club

Comments are closed.