KLABU ya Yanga imetangaza kuanza kuchangisha fedha kwa ajili ya kujikwamua katika hali ngumu waliyonayo kipindi hiki.
Nilimuona Kaimu Katibu Mkuu wa Yanga, Omary Kaaya akiwaambia wanachama na wapenzi wa Yanga kwamba wanatakiwa kuacha kulaumu na badala yake mara moja kuanza kuichangia klabu yao ili kuhakikisha mambo yanakwenda vizuri na wanajiondoa katika hali ngumu waliyonayo.
Katika kauli zake, Kaaya anawakumbusha wanachama wa Yanga kuchangia kwa kuwa hali ni mbaya na wao wamekuwa wakilaumu tu lakini sasa ni wakati wa wao kuonyesha mapenzi yao kwa vitendo.
Kama utaingia ndani ya kile ambacho amekuwa akikisema Kaaya, naweza kusema ni sahihi kabisa kwa wanachama na wapenzi wa Yanga kuonyesha mapenzi yao kwa dhati.
Kuchangia klabu yao ni jambo sahihi kabisa na inatakiwa kuwa hivyo kwa kuwa ndiyo mapenzi ya dhati. Lakini kuna mengi kadhaa ya kujiuliza ambayo yalitakiwa kufanyiwa kazi au kutangazwa kabla ya michango ambayo wametaka wapewe na wanachama au mashabiki.
Moja, suala la michango ambayo iliwahi kuchangishwa miezi kadhaa iliyopita na Klabu ya Yanga na mwisho ikaelezwa waliochanga walikuwa ni watu wachache sana, zilizopatikana ni kiasi gani? Na kama ni kiasi fulani, vipi zilitumika kufanyia nini? Na kama ni hivyo, msaada wa kile kidogo kilichopatikana, kiliisaidiaje Yanga?
Nauliza, baada ya wale wachache waliochanga, uongozi uliwashukuru? Pia wakati unaanza kuchangisha uliwakumbuka waliochanga wakati ule kwa kuwashukuru tena na kuwaomba msaada zaidi?
Haya yanaweza kuwa ni maswali ya awali ambayo tunaweza kujiuliza. Lakini kunaweza kuwa na mengi sana ya kujiuliza hasa kuanzia kwa Kaaya ambaye alikuwa akihusika na suala la masoko katika klabu hiyo.
Yanga ni ‘brand’ kubwa, vipi hadi sasa haina wadhamini wengi wa kutosha ambao wanaweza kuisaidia kufanya mambo yake vizuri.
Wale Macron ambao Yanga walieleza wataanza kuvaa jezi zao, tunajua ni kampuni kubwa kabisa. Vipi leo hakuna wanachoingiza ndani ya Yanga na kama kipo ni kiasi gani? Kwa kipindi hiki kimesaidia vipi, na kama hawapo, vipi wanachama au mashabiki hawajawahi kutangaziwa kama ilivyokuwa walitangaziwa ukionekana ni wakati mzuri na neema ndani ya Klabu ya Yanga?
Mchango kipindi hiki wakati ambao Yanga hawaaminiki na kuna maneno mengi yanazungumzwa wakituhumiwa kufuja baadhi ya fedha.
Wakati unawaomba wanachama na mashabiki michango lazima ufafanue, kwamba tuhuma zilikuwa hivi na vile. Mfano, Clement Sanga alielezea kuhusiana na matumizi yalivyokuwa baada ya kutuhumiwa, halafu akajiuzulu. Sanga hayupo tena.
Lakini bado kuna jambo ambalo Yanga walitakiwa kulifanyia kazi hasa na huenda lingewapunguzia kuanza kuomba michango. Hapa nazungumzia ada za wanachama wao ambao baadhi wamekuwa hawalipi.
Inaonekana wengi hawalipi ada zao, basi kupitia matawi yao lingefanyiwa kazi na kuisaidia klabu. Hata kama wangepata asilimia 60 ya madeni ya ada, ninaamini ingesaidia kwa kiasi kikubwa.
Mwisho hata ule udhamini wa kampuni ya maji tunaouona kwenye matangazo ya Klabu ya Yanga, una faida? Yanga inalipwa kiasi gani.
Mwisho mwisho kabisa, namkumbusha Kaaya kuwa kuendelea kuomba misaada ni kukosa ubunifu kwa kuwa Yanga ina kila sababu ya kupata nafasi ya kujiendesha na kujiendeleza kwa fedha zake yenyewe na si kuomba.
Kipindi cha kutembeza mabakuli kwa klabu kama Yanga ni uvivu wa matumizi ya akili. Kinachotakiwa ni ubunifu zaidi na zaidi ili kupata wadhamini, kupata wanachama kwa wingi zaidi, kuingiza fedha nyingi za matangazo na kadhalika.
Najua haitakuwa rahisi, lakini kama kiongozi unatakiwa kukutana na mambo magumu na kuleta mabadiliko. Kutaka vilaini ni kuonyesha uwezo mdogo hivyo, Yanga iachane na michango, viongozi wafanye kazi ya ziada kuikwamua klabu hiyo kwa ubunifu na mipango sahihi.
NA SALEH ALLY, HOJA YANGU, CHAMPIONI IJUMAA
Comments are closed.