The House of Favourite Newspapers

Yanga Yampa Mkataba wa Kufuru Luis Miquissone Baada ya Kuvamia Dili la Simba

0
Luis Miquissone.

WAKATI Klabu ya Simba ikiendelea kupewa asilimia nyingi za kumrejesha winga wao wa zamani raia wa Msumbiji, Luis Miquissone, uongozi wa Yanga, umedaiwa kuvamia dili hilo na kutaka kumshusha mwamba huyo Jangwani.

Luis aliachana na Simba Agosti 26, mwaka jana na kujiunga na timu ya Al Ahly ya Misri ambayo baadaye ilimtoa kwa mkopo katika timu ya Abha Club ya Saudi Arabia na huko ameshindwa kuwika.

Chanzo chetu kutoka Simba kimeliambia Championi Jumamosi kuwa, baada ya Yanga kusikia kuwa Luis anaomba kurejea Simba, ilituma watu wake kwa ajili ya kuzungumza na uongozi wa mchezaji huyo.

Yanga walikubali kutoa dau la kufuru na kumlipa mshahara wa maana ambao unakaribiana na ule anaolipwa kwa sasa Al Ahly lakini Luis alichomoa na kusema ana mapenzi na Simba pekee.

“Kuna jambo zito linaendelea kwa Miquissone na mameneja wake, maana sisi kama Simba tayari tumeshafanya kinachostahili ili kumrejesha Miquissone ambaye kwa asilimia kubwa ameonyesha kuhitaji kuja kikosini mwetu ili kuongeza nguvu.

“Habari zinazotuchanganya ni kuwa tumesikia wenzetu nao wamezunguka na kwenda upande wa menejimenti yake na kutoa ofa yao ambapo wameonyesha nia ya kumtaka mchezaji kwa gharama yoyote hasa baada ya kusikia makubaliano yetu na Al Ahly.

“Nina imani kama mchezaji hatabadilisha kauli zake za awali basi tutaungana naye muda wowote baada ya sisi kumalizana na uongozi wake ambao ndiyo kikwazo kilichobaki kwa sasa baada ya kuzungumza mambo yote ya uhamisho na gaharama za mshahara wake na mchezaji,” kilisema chanzo hicho.

Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally alizungumzia hilo la usajili na kusema kuwa: “Ni lazima tukifanyie maboresho makubwa kikosi chetu katika usajili huu wa dirisha dogo lakini siwezi kukutajia majina ya wachezaji ambao tunawaangalia hadi pale tutakapokamilisha usajili wetu.”

Stoti na Musa Mateja

BUMBULI ATINGA KWA MKAPA, ATOA KAULI HIZI ZA KIBABE, AMMWAGIA SIFA CLEMENT, ATUMA UJUMBE MZITO…

Leave A Reply