The House of Favourite Newspapers

ZARI KUHAMA KIBABE MJENGO WA MONDI

DAR ES SALAAM: MWENYE pesa si mwenzako! Hayo ni maneno ya Wimbo wa Mtu Pesa wa Bendi ya The African Stars ‘Twanga Pepeta’ ambayo yanaakisi jeuri ya fedha iliyooneshwa na mwanamama Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’ huko Afrika Kusini ‘Sauz’.

 

Iko hivi, Zari ambaye ni mzazi mwenza wa staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ au ‘Mondi’ anatarajia kuhama kibabe kwenye mjengo wa kifahari ambao msanii huyo alimnunulia wakati mapenzi yao yalipokuwa motomoto.

TUJIUNGE UGANDA

Kwa mujibu wa mitandao ya nchini Uganda anakotokea Zari, mwanamama amefikia uamuzi huo baada ya kuona meneno yamekuwa mengi kumhusu yeye na nyumba hiyo ya Diamond hususan kutoka kwa mashabiki wa Tanzania.MANENO YENYEWE… Gazeti la Ijumaa limeshuhudia maneno hayo ambayo yanatajwa kumkera Zari kuwa ni yale yanayomsema kuhusu kumuingiza mpenzi wake mpya maarufu kwa jina la King Bae katika nyumba ya mwanaume mwenzake (ya Diamond).

 

“Zari anajifanya ana pesa, lakini hana lolote, anamuingizaje mwanaume kwenye nyumba ya Diamond?” Hiyo ilikuwa ni sehemu ya jumbe zilizorushwa mitandaoni. Jumbe nyingine zilizorushwa mitandaoni zilimshauri Diamond aandae nyaraka za nyumba hiyo na kwenda kuiuza kwa sababu haiwezekani anunue yeye kwa ajili ya watoto wake, Tiffha na Nillan halafu Zari aingize mwanaume mwingine.

 

Mbali na hilo, kuna mashabiki wengine walikwenda mbali zaidi kwa kusema Zari amezoea kuwapiga wanaume kwa kuomba kujengewa au kununuliwa nyumba kisha mapenzi yanapoisha ananufaika nazo. “Alifanya hivyo kwa Ivan Semwanga (marehemu mumewe), akafanya pia kwa Diamond na hata hii mpya ambayo nasikia anataka kuhamia, ni ya King Bae,” aliandika mdau katika mtandao wa Instagra.

TUREJEE UGANDA KIDOGO

Mitandao hiyo ya Uganda imeeleza kuwa, baada ya Zari kukereka na maneno hayo, kwa sababu yeye kwake fedha si tatizo, ameamua kununua nyumba hiyo mpya ili kuwaonesha jeuri mashabiki wake kwamba yeye pesa siyo tatizo kwake. Japo gharama zake bado hazijapatikana kwa urahisi, lakini imeelezwa kuwa nyumba hiyo ni ya gharama kubwa na ya kifahari zaidi.

 

Imeelezwa kuwa nyumba hiyo ni ya kifahari na mrembo huyo tayari ameshaagiza samani za ndani za kisasa na kuonesha kwamba hataki utani, hatahamia na kitu chochote kilichonunuliwa na Diamond. “Yaani pale mtoto wa kike atahamia yeye kama yeye, atakuwa anaonesha kwamba pesa anazo, nyumba ipo mahali pa kishua, ina kila kitu ndani, mapambo ya kisasa, yaani ni nyumba ya kistaa,” iliandika mitandao mbalimbali ya Uganda.

YAIBUA GUMZO

Mapema wiki hii, mrembo huyo wa Kiganda kupitia kipengele cha Insta Stories kwenye Mtandao wa Instagram, aliweka kipande cha video kinachoonesha fundi akiweka mapazia katika nyumba hiyo mpya.

 

MARA PAAH! KING BAE…

Kama hiyo haitoshi, Zari aliweka picha nyingine akiwa mbele ya nyumba hiyo akiwa na King Bae huku kibao cha kuonesha nyumba hiyo imeshanunuliwa (sold). Kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii, picha hiyo iliibua gumzo si la nchi hii ambapo wapo waliompongeza mrembo huyo, lakini wengine walimponda kwa kusema haiwezi kuwa yake bali atakuwa amenunuliwa na mpenzi wake huyo mpya.

 

WAGANDA WAMTETEA

Hata hivyo, Mitandao ya Uganda imeeleza kuwa, mrembo huyo ameinunua nyumba hiyo kwa fedha zake na kwamba suala la kwamba hana uwezo wa kununua halina mashiko. Mrembo huyo anatajwa kuwa na utajiri wa kutosha kwani anamiliki maduka na shule (The Brooklyn Schools) huko Sauz.

 

Inaaminika kuwa, marehemu mume wake aliyekuwa na utajiri wa Dola za Kimarekani milioni 8.8 (zaidi ya shilingi bilioni 20), alimpa nusu ya utajiri huo yeye pamoja na watoto aliomuachia.

MADILI YA UBALOZI KIBAO

Kama hiyo haitoshi, mrembo huyo amekuwa akilamba madili makubwa ya ubalozi ambayo yanamuingizia fedha nyingi, jambo ambalo kweli linaonesha ni dhahiri kwamba hawezi kushindwa kununua nyumba Sauz.

 

MAGARI KAMA YOTE

Zari anatajwa pia kumiliki magari mengi ya kifahari yakiwemo Mercedes-Benz, Range Rover, Hummer H2, Lamborghini na Chrysler ambayo ameandika majina yake. Mbali na nyumba na nyumba hizo mbili za Johannesburg, Afrika Kusini, Zari anatajwa kumiliki nyumba nyingine ya kifahari iliyopo maeno ya Pretoria nchini humo na Kampala, Uganda.

Comments are closed.