The House of Favourite Newspapers

Mambo 10 Yanayofanya Mtu Kunenepa

Na Mwandishi Wetu/GPL
MIONGONI mwa maswali ya wasomaji wetu ni juu ya watu ambao wametumia njia mbalimbali ili kuondoa uzito au unene kupita kiasi bila mafanikio. Leo tutajadili hilo.

Unene kupita kiasi ni nini? Haya ni mafuta yaliyozidi kuzunguka eneo la tumbo na sehemu nyingine za mwili. Unaweza kutokea kwa watoto, vijana na watu wazima hata wazee wa jinsia zote. Mwili wa binadamu una seli bilioni 50-200 za mafuta zilizogawanyika kwenye mwili wa binadamu.

Kwa wanawake zipo sana maeneo ya matiti, nyonga (hips), kiuno na kwenye makalio. Kwa wanaume seli zipo sana kwenye kifua, tumboni na kwenye makalio. Mafuta ya tumbo yanayofanya kitambi hukusanywa kwa njia kuu mbili, ya kwanza ni mafuta
kutoka kwenye tishu zilizo chini ya ngozi na ya pili ni kutoka kwenye ogani za ndani kama moyo na kongosho.

Sababu kubwa ya unene ni kukosekana ulingano wa nguvu (kalori) kama vile mtu kula vyakula vinavyotia nguvu sana kuliko jinsi anavyoweza kutumia na kutoa kama taka mwili.

Sababu zingine ni kuwa na chembe za urithi za unene kutoka kwa wazazi. Kuna sababu za kimazingira na nyingine zisizojulikana. Vitu kama kukosa usingizi na sababu nyingine zinachangia kuendelea kuwepo kwa unene au kitambi ambacho kinaweza kuashiria maradhi ya moyo, kisukari na baadhi ya magonjwa ya saratani.

Mchanganuo wa sababu 10 zinazofanya mtu kuendelea kuwa mnene au kitambi: 1.Kadiri unavyozeeka, mwili wako unabadili jinsi unavyo ongezeka na kupunguza uzito. Jinsi zote; za kike na kiume, hupatwa na kupungua kwa utendaji wa kimetaboliki, kutia ndani kiasi cha kalori zinazohitajika kwa mwili kufanya kazi kwa ukawaida.

Zaidi ya hayo wanawake hupatwa na kukoma kwa hedhi, ikiwa wanawake wataongezeka uzito, mara nyingi uzito huo huwa kwenye matumbo yao.
Wakati wa kukoma kwa hedhi, uzalishaji wa homoni za Istrojeni na Projesteroni hupungua. Wakati huo huo homoni ya Testosteroni huanza kupungua kidogo kidogo.

Mabadiliko ya homoni hufanya wanawake wengi kuendelea kubeba uzito mwingi kwenye matumbo yao. 2. Kutofanya mazoezi kwa usahihi. Mazoezi ya kulala chali na kuinua mwili kuanzia kiuno hadi kichwa Crunches siyo mazoezi yatakayokusaidia kuondoa unene au kitambi. Badala yake fanya mazoezi ya stamina yatakayo kufanya utumie nyama Muscles za tumbo, mgongo, nyonga na
sehemu zingine za mwili.

Kufanya mazoezi ya namna hii kutasaidia kuunguza/ kutumia kalori nyingi mwilini na hivyo kufanya mafuta yaliyo maeneo ya tumbo kutumika pia. Mazoezi ya kukaa kwa muda jinsi fulani kama unapiga pushapu kitaalamu hujulikana kama Plunk , ndiyo mazoezi yanayofaa kwa kuwa huhusisha matumizi ya nyama za mikono, miguu na makalio.

Kukimbia kila siku ni mazoezi bora kwa mwili na moyo wako ingawa mazoezi kwa ajili ya moyo wenye afya peke yake hayawezi kusaidia maeneo ya kiunoni na kutoa kitambi.

Itaendelea wiki Ijayo…

 

Comments are closed.