The House of Favourite Newspapers

Hatua Nne za Ugonjwa wa Vidonda vya Tumbo

0

MGONJWA wa vidonda vya tumbo katika hatua ya kwanza asipopata tiba, tindikali nyingi iliyozalishwa tumboni hushuka na kuingia kwenye utumbo mdogo na kuharibu mfumo wa mmeng’enyo au usagaji wa chakula kwa kuwa vimeng’enyo vya utumbo mdogo hushindwa kufanya kazi kwenye mazingira ya tindikali.

Hali hii husababisha kuharibika kwa uteute wa sehemu hii ambao ndiyo ulinzi wa utumbo mdogo na matokeo yake ni mtu kuwa na vidonda tumboni pia kwenye utumbo mdogo yaani duodenal ulcers. Kuna dhana iliyozoeleka kuwa vidonda vya tumbo huathiri zaidi mfuko wa kuhifadhia chakula yaani tumbo stomach.

Dhana hii si kweli kwani sehemu inayoathiriwa zaidi na tatizo hili ni sehemu ya kwanza ya utumbo mdogo ijulikanayo kama duodenum. Dalili ya mwanzo  kabisa ya ugonjwa ni ule uvimbe tuliosema unajitokeza  sehemu ya ndani ya tumbo, tumbo kujaa gesi, kichefuchefu cha mara kwa mara, kiungulia kikali na kutapika kwa baadhi ya wagonjwa.

HATUA YA PILI Hatua ya pili vidonda hujitokeza sehemu zenye uvimbe na taratibu vidonda hivyo huongezeka na kuwa vikubwa.Ni katika hatua hii mgonjwa huwa na maumivu makali ya tumbo yanayodumu kwa muda mrefu, kujaa gesi, kukosa hamu ya kula, choo kuwa kigumu au kukosa choo kwa muda mrefu. Hali hii ya kukosa choo kwa
muda mrefu hujulikana kama chronic dispepsia -yaani kushindwa kufanyakazi kwa mfumo wa kusaga au kumeng’enya chakula kutokana na tindikali nyingi inayozalishwa tumboni.

Tindikali hiyo huingia kwenye mzunguko wa damu, mgonjwa hujisikia uchovu na kizunguzungu, homa hasa nyakati za jioni na pia mgonjwa hupoteza uzito wa mwili Katika hatua hii tindikali husababisha magonjwa ya ini na figo kwa kuwa tayari iko katika mfumo mzima wa mwili kupitia mzunguko wa damu.

HATUA YA TATU

Ni kwamba vidonda vikubwa hupasua mishipa midogo ya damu na kusabababisha damu kuvia tumboni na kubadilisha rangi ya choo cha mgonjwa kuwa ya kahawia. Damu nyingi ikivia tumboni mgonjwa hutapika na kuharisha damu, hali hii husababisha mgonjwa kuishiwa damu mara kwa mara, maumivu makali ya tumbo huongezeka, homa, maumivu ya viungo na kukosa hamu ya chakula.

HATUA YA NNE

Hatua ya nne ya vidonda vya tumbo ni mtu kukumbwa na saratani ya utumbo na ni hatua ambayo ni ya hatari sana kwa kuwa vidonda hutengeneza tundu katika tumbo au utumbo mdogo na kusababisha kuoza kwa viungo muhimu vya ndani na matokeo yake ni saratani au kansa ya utumbo.

VIPIMO

Baadhi ya vipimo vitachukuliwa ili ithibitike kwa uhakika kama ni vidonda vya tumbo. Vipimo hivi ni kama vile kipimo cha damu, kipimo cha pumzi, kipimo cha choo.  Kipimo cha damu blood test kinaweza kutambua kama bakteria H. pylori yupo.

Pia, kama mtu alikuwa anatumia antibayotiki au proton pump inhibitors , kipimo hiki  kinaweza kutoa majibu yasiyo sahihi. Kipimo cha pumzi breath test kinaweza kupima vidonda vya tumbo. Katika kipimo hiki, atomu ya kaboni mnunurisho yaani radioactive carbon atom hutumika kuchunguza H. pylori .

Kipimo hiki cha pumzi ambacho ni uvumbuzi wa hivi karibuni, kina usahihi zaidi kwa asilimia 95.  Kipimo cha choo stool antigen test hutumika kutambua kama H. pylori yumo ndani ya kinyesi na hutumika kufahamu ni kwa jinsi gani matibabu yamefanikiwa kuondoa bakteria.

Kipimo cha X-Ray Upper gastrointestinal X-Ray,  hiki hutazama tumbo na duodeni. Na Upper GI X-Ray hutumika tu kutambua baadhi ya vidonda.  Endoscopy ni kipimo ambacho kwa uangalifu sana, daktari ataingiza mrija mwembamba wenye kamera ndogo sana unaoitwa endoscope chini ya koromeo kupitia koromeo hadi kwenye tumbo, huko anaweza kuona sehemu ya juu ya eneo la mmeng’enyo wa chakula kwenye monitor na kutambua kama kidonda kipo.

MATIBABU & KINGA

Mambo ya kuzingatia ili kujikinga na vidonda vya tumbo: ni kula polepole, hii itaongeza umeng’enywaji mzuri wa chakula. Usifanye kazi nzito baada ya kula; punguza mawazo na ishi maisha ya furaha; usivute sigara; usinywe pombe; usitumie dawa kama vile aspirin kwa muda mrefu; chunga matumizi yako ya kahawa; osha mikono yako kwa maji ya uvuguvugu baada ya kutoka msalani

Leave A Reply