KELELE za malalamiko kuhusu soka la Tanzania zimekuwa nyingi na kubwa, lakini ukijiuliza sana unaweza kuona kuna mahali tunalaumu bila ya kujua nani tunayemlaumu.
Lawama tumezaliwa nazo, tena wengi tumekuwa watengeneza lawama wakubwa tena zile za kuvutia kiasi cha kupendwa na watu wengi katika mitandao ya kijamii, tukibadili lugha na mitindo ya kuandika.
Watanzania wengi ni wepesi wa kukosoa hata yale mambo yanayoonekana kwanza yapongezwe halafu yakosolewe kwa kurekebishwa kidogo tu.
Ujuaji ndiyo uliotufanya tumwone Leodegar Tenga hafai katika uongozi na alipopewa mwingine nadhani tukaona bora yule ya mwanzo, tabia hii tunayo hadi katika siasa.
Kwamba tunaishi kwa mazoea na hatupo tayari kukubaliana na ukweli wa mambo wakati mwingine. Kuna kizazi hiki cha sasa ambacho ni cha wasomi wanaojua kila kitu, hawa ni watu wazuri ila hawajui wafanyalo.
Vijana hao wengi wamejaa katika mitandao ya kijamii wakiwa makini katika kukosoa kila kitu, najua wana haki yao, nawapongeza na nakubali kuhusu uwezo wao kwani wanaleta changamoto mpya.
Lakini nyuma ya pazia, kinachowafanya wawe hivyo ni uelewa wao katika mambo yanayoendelea dunia ya kwanza, lakini hawapaswi kuishia kukosoa peke yake, bali kutoa njia mbadala.
Kuna mambo mengi yanayoweza kuchangia mafanikio ya soka letu lakini kuziachia taasisi husika peke yake hatutaweza kupiga hatua. Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) haliwezi kumfikia kila mtoto wa Tanzania kumuhamasisha acheze soka.
Kila mmoja sasa aache kuona jukumu la soka la vijana si lake hata kuanzia ngazi ya mtaa, tunaweza kufanya kitu cha maana na tukafanikiwa.
Nenda mtaani kwako katika kiwanja cha wazi kawatazame watoto wanavyocheza soka kwa shida na utazame ni kwa namna gani utaweza kuwasaidia hasa katika vifaa.
Ni watoto wachache sana wanaolazimishwa kucheza soka katika jamii zetu, kwani wengi wao hupenda wenyewe mchezo huu na kujituma bila ya kuhimizwa mara kwa mara.
Unatoa mfano wa England au Hispania inavyopiga hatua lakini unasahau mazingira yao yalivyo na sisi huku jinsi tulivyo na hata nchi kama Nigeria na Cameroon pia ni tofauti na sisi.
Wenzetu soka ni ajira na wana akademi nyingi zenye uhusiano na klabu kadhaa za Ulaya wakiamini wanafanya biashara ya wachezaji chipukizi, lakini sisi tunahangaika hapa kwani hakuna akademi ya kueleweka ya watoto.
Akademi nyingi zinaweza kuchukua watoto kuanzia kidato cha kwanza na wale wa shule za msingi hawana nafasi sehemu nyingi. Hapo ndipo tunapoanza kukwama katika maendeleo ya soka letu.
Vijana wetu wengi wanajifunza soka kuanzia sekondari, hii ni hatari. Huko mitaani tuwasaidie kwa kuwapa vifaa vya michezo na mnaweza wadau mkajipanga na kusaidia timu ya mtaani kwenu.
Mkaitafutia michuano ikacheza na kutoa wachezaji kwenda mahali kwingine na mchezaji huyo akifika mbali, basi wewe utakuwa mmoja wa msaada mkubwa kwake na siyo kuishia kupayuka mitandaoni.
Soka la Tanzania ni letu sote na tusitumie muda mwingi kulalamika bila ya kuwa na majibu ya masuluhisho ya matatizo yetu katika kuelekea mafanikio ya soka.
Tukibaki kulaumiana, tutalaumiana milele na hakuna kitakachoendelea katika soka letu na ni hatari kufananisha soka letu na mambo yanayotokea England, huo ni upuuzi uliopitiliza japokuwa tunaweza kuiga kidogokidogo.
Vijana tupambane kuokoa soka letu na tujione ni sehemu ya kuelekea mafanikio na tusiache kazi hii kwa kikundi fulani cha watu, tutafeli.