The House of Favourite Newspapers

Samatta achukua ubingwa Ubelgiji, apewa mbuzi

 

MBWANA Samatta ndiye Mtanzania wa kwanza kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya Ubelgiji sasa baba yake, Mzee Ally Samatta amepanga kumchinjia mbuzi kijana wake ili kusherehekea ubingwa huo.

 

Usiku wa kuamkia jana Ijumaa, Klabu ya KRC Genk anayochezea Samatta ilitoka sare ya bao 1-1 na Anderletch katika mchezo wa playoff katika ligi hiyo ambapo matokeo hayo yameifanya Genk kufikisha alama 51 ambazo haziwezi kufikiwa na timu zingine huku kila timu ikisaliwa na mechi moja.

 

Samatta ambaye alijiunga na Genk mwaka 2016 akitokea TP Mazembe ya DR Congo, huu umekuwa msimu mzuri kwake pale Genk kwani awali hivi karibuni tu alitwaa Tuzo ya Mchezaji Bora Mwenye Asili ya Afrika ambaye anacheza ligi ya Ubelgiji. Akizungumza na Championi Jumamosi, mzee

Samatta ambaye amekuwa akiwashukuru Watanzania kutokana na sapoti wanayompa Samatta alisema kuwa, amefurahishwa na mtoto wake kuendelea kufanya vizuri barani Ulaya baada ya kufanikiwa kushinda ubingwa wake wa kwanza akiwa na Genk.

 

“Binafsi siwezi kukasirika maana hapa nina furaha kubwa, namuombea dua siku zote kwa Mungu aweze kumfungulia milango baraka, uzuri amekuwa akinisikiliza na anajielewa kwa kile anachofanya ndiyo jambo kubwa la kushukuru ingawa haikuwa rahisi kwao kutokana na ushindani wa ligi yao ilivyo.

 

“Unajua jana (juzi) baada ya ile mechi kuisha sikupata usingizi kwa furaha na ilibaki kidogo nivunje kitanda, nimepanga akirudi nchini nimchinjie mbuzi ale hapa nyumbani na rafiki zake kwa sababu jogoo nitachinja kwa ajili ya kula yeye mwenyewe kwa kuwa nimekuwa nikifanya hivyo kila anapokuwa amefanya vizuri,” alisema mzee Samatta

Ibrahim Mussa, Dar es Salaam

Comments are closed.