The House of Favourite Newspapers

Niliolewa na Mganga kwa tamaa ya cheo kazini-22

0

ILIPOISHIA:

Kwa kweli jibu lilikuwa gumu kupatikana na kuuliza niliogopa kuudhiana na shoga yangu, niliamua kukaa kimya mpaka nitakapoondoka na hata mjini sitamwambia mtu niliyoyaona kwa mzee Sionjwi hata wazazi na ndugu wa Rose niliapa sitawaambia kitu chochote kuhusiana na Rose niliogopa kumuudhi mzee Sionjwi na kukosa tiba ya matatizo yangu.

SASA ENDELEA… 

Ajabu Rose hakuonesha mabadiliko yoyote zaidi ya kunenepa na kupendeza nilijiuliza ameridhika na nini, maisha kule kijijini hayakuwa mazuri sana vitu vingi hawakupata zaidi ya kula visivyokuwa na mafuta wala kiwango cha juu japo katika sayansi chakula walichokula kilikuwa bora kuliko tulivyokuwa tukila mjini vingi vilipoteza ubora.

Mzee Sionjwi alirudi saa nane akiwa na kapu lake lililokuwa limejaa dawa, alipokuwa akija kwa mbali nilijikuta nikimuona kiumbe mpya kwangu kama mtu niliyewahi kusikia historia yake na kuwa na hamu ya kumuona. Kila nilivyomwangalia sikummaliza.

Umri wa yule mzee kwa hesabu za haraka alikuwa anakimbilia miaka 75, ukimuangalia unaweza kusema hana nguvu lakini akikushika hasa katika mchezo wa kikubwa utamjua yule mzee ni nani hachoki pia ni mjuzi wa kukufanya ufurahie tendo lile hata usitake ateremke haraka.

Nilimwangalia toka alipotokea mpaka alipofika karibu yangu, alipofika tulipokuwa tumekaa nilimsikia akisema.

“Aah, kumbe tuna ugeni?”

“Ndiyo babu  shikamoo,” nilimjibu.

“Marahaba, karibu.”

“Asante babu.”

“Vipi umefika zamani?”

“Muda tangu asubuhi.”

“Karibu, si unajua tena kazi zetu kila kukicha tunatengeneza dawa basi lazima tudamke alfajiri kuingia porini kutafuta dawa. Lakini wenyeji wako si umewakuta?”

“Nashukuru babu wamenipokea vizuri.”

“Rose kaniletee maji ya kunywa.”

Rose alinyanyua na tumbo lake huku akiuma meno kufuata maji ya kunywa ya mumewe mzee Sionjwi.

“Rose mtoto mmoja umechoka hivyo wakifika kumi je?”

Maneno ya mzee Sionjwi yalinistaajabisha kuhusu kumzalisha watoto kumi Rose, nilijiuliza hao watoto kumi wa Rose na wengine sijui watakuwa wangapi na nini hatima ya maisha yao. Niliamini babu yule pamoja na umri mkubwa bado aliweza kufikisha watoto hata 30 lakini nini urithi wa watoto kama mzee Sionjwi atakufa.

Pia nilimuonea huruma Rose mtu mwenye elimu yake japo hakufikia elimu yangu lakini elimu ya kidato cha sita ingeweza kumpa mwanga wa kuchagua maisha ya kuishi na siyo kuolewa na mganga asiye na kitu chochote ambacho kingeweza kumsaidia maishani pindi mumewe atakapofariki.

Kuna kitu ambacho niliamini Rose alisikiliza ladha ya mapenzi aliyopewa na mzee Sionjwi, kama nilivyosema ukikutana na yule mzee kimwili kama huna moyo mgumu kama umeolewa lazima utaisaliti ndoa yako. Hata sikujua babu alikuwa na nini cha ziada kuliko wanaume wengine.

Lakini japo mzee anajua kukata kiu ya mapenzi lakini bado ulitakiwa mtu kujiuliza ukifuatacho faida na hasara ipi imezidi upande mmoja. Sikutaka kuhoji sana nililiacha kama nilivyolikuta japo nilijawa na mawazo mengi akilini mwangu.

Kila nilivyokuwa nikimuangalia Rose jinsi Mungu alivyomuumba na uamuzi wa kuolewa na kikongwe kama mzee Sionjwi sikupata jibu. Niliamua bora niachane naye na kuendelea na kilichonipeleka pale. Baada ya muda Rose alirudi na kombe kubwa la maji nakumbuka nililileta mimi baada ya kutumwa na mzee Sionjwi nimnunulie.

Mmh, makubwa Rose alipofika mbele ya mzee Sionjwi alipiga magoti na kumpa maji kwa heshima zote. Mzee Sionjwi alichukua maji ya kunywa huku Rose akiwa bado amepiga magoti.

Baada ya kunywa Rose alipokea kikombe huku mzee Sionjwi sijui nimwite dume la mbwa au jogoo la mtaa kila kuku jike wake, akisema…

“Asante mpenzi.”

“Asante kwa kushukuru mpenzi.”

Rose alinyanyuka na kuelekea ndani kurudisha kikombe, baada ya kunywa maji alimtuma bi mkubwa kwenda kumwekea maji ya kuoga. Aliniacha na baadhi ya wakeze na kwenda kuoga, Rose alirudi na kukaa huku akishika kiuno na kukunja uso.

“Vipi tena shoga?” nilimuuliza.

“Mmh, kiuno.”

“Kimefanya nini?”

“Tangu jana na kila nikimweleza mzee Sionjwi anasema nisubiri zamu yangu ndiyo anipe tiba.”

“Kwani zamu yako lini?” Nilijitia umbea kuuliza yasiyonihusu.

“Leo usiku.”

“Sasa tiba mpaka ifike zamu yako?”

“Utamuweza mzee yule ngono itamuua anapenda kama chakula.”

Nilitamani kucheka kusikia hata wakeze wanajua kuwa bwana wao anapenda sana ngono.

“Si mtamuua ninyi wote wanne tena wote mpo kamili.”

“Kile kizee wanga tu hakina lolote.”

“Heheheheheheheeee….Rose utanivunja mbavu miye,” nilijikuta nacheka bila kupenda.

“Si utani Efrazia kama siyo wanga ni nini? Mtu kikongwe kama yule kuweza kugawa dozi kwetu sote tena si ya kitoto na bado yupo fiti.”

JIUNGE NA GLOBAL BRAKING NEWS UPATE HABARI KEMKEM ZA UCHAGUZI MKUU

globalbreakingnews.JPG

Leave A Reply