The House of Favourite Newspapers

Acha kumchezea, kama humtaki

0
Attractive couple having an argument on couch at home in the living room
Attractive couple having an argument on couch at home in the living room

Habari za leo wapendwa wasomaji wa safu yetu hii inayozidi kujizolea umaarufu. Ni imani yangu kuwa mambo yanakwenda sawa na kila mmoja wenu anaelewa kuhusu mada mbalimbali ninazowaletea.

Mara nyingi nimekuwa nikizungumza zaidi kuhusu wanawake wenzangu, lakini leo nimeona acha niwageukie akina baba kidogo, kwa sababu yale yote tunayoelekezana kila siku yanalenga kuimarisha ndoa na uhusiano wetu, ambao wanaoubeba ndiyo hawa wenza wetu tunaopenda kuwaita kichwa cha nyumba.

Hapa nizungumzie kuhusu uhusiano. Tunatambua kuwa huwezi kuwa mke au mume bila kwanza kuanza na mwenzi wako katika urafiki, uchumba na hatimaye ndoa. Lakini ukiangalia maisha ya sasa, hasa mijini, kati ya wanaoishi chumba kimoja, kwa maana ya kupika na kupakua zaidi ya asilimia 75 ni ambao hawajaoana.

Yaani wanaishi kwa miaka mingi kama marafiki tu, kisingizio kikubwa cha kinababa wengi ni kuwa hawajajipanga, eti wakiwa tayari watafunga ndoa, kana kwamba kuoa kunahitaji mamilioni ya shilingi.

Akina baba wengi wamekuwa wakijifikiria wao tu, kwani ni ngumu kwao kujua kuwa kadiri penzi linavyochukua muda mrefu ndivyo pia umri unavyozidi kuwa mkubwa na kwetu sisi wanawake, tunavyokua wakubwa kiumri ndivyo uzuri wetu nao unapungua.

Hivi, kama kweli unampenda mpenzi wako na mko pamoja kwa miaka kibao, kuna tatizo gani kumuoa? Huoni kama kwa kukaa kwako kimya kwa muda mrefu unamkosesha mwenzio bahati yake?
Lakini hata hivyo, tatizo la wanaume kukaa muda mrefu na wanawake bila kuwaoa linachangiwa kwa kiasi kikubwa na sisi wanawake wenyewe. Tuko rahisi sana kukubali kusubiri bila kujua kuwa kadiri tunavyoendelea, ndivyo na thamani yetu kama akina dada inaisha.

Inavyoonekana, hatujui kama kuna hasara ya kuendelea kusubiri ndoa. Ukiwa na mwanaume kwa muda mrefu ni rahisi kukuchoka, hasa kama mtakuwa na migogoro. Hapo unampa kisingizio cha kukuacha kwa kile wanachosema, eti labda baada ya kukupima anakuona hufai.

Wakati mwingine hiyo hutokea anapokuwa  amepata kimada huko pembeni ambacho kikiwa makini anaweza kumuoa na wewe kuendelea kuwa kimada mzoefu.

Pia wanawake tuna tatizo la uvumilivu kupita kiasi na wepesi kusamehe, ndiyo maana tunakubali kukaa na maumivu ya kutoolewa kwa kipindi kirefu bila kuelewa jambo hilo linatumiwa na wanaume kutuadhibu.

Ninachowaomba wanaume, ni kuweka imani yao ya kidini mbele, wawe na muda mfupi na wenza wao ili waamue kama ni kufunga nao ndoa au la ili kuwapa nafasi ya kufanya mambo mengine.

Kaa na ujiulize utajipanga mpaka lini, lakini pia kama unampenda kwa dhati mpe nafasi auone upendo wako kwa kumuoa.

SOCIAL MEDIA ZETU:

KWA HABARI ZA KITAIFA, KIMATAIFA, MASTAA NA MIKASA YA KUSISIMUA

INSTAGRAM: @Globalpublishers

TWITTER: @GlobalHabari

FACEBOOK: @GlobalPublishers

SUBSCRIBE YOU TUBE: GlobalPublishers

GLOBAL TV ONLINE: www.globaltvtz.com

HADITHI ZA KUSISIMUA NA MBINU ZA UJASIRIAMALI, ERIC SHIGONGO FACEBOOK PAGE: @shigongotz

Leave A Reply