Ajibu Aingia Kwa Dk Shika, Apeleka Shangwe Yanga SC
MSHAMBULIAJI tegemeo wa Yanga, Ibrahim Ajibu amemtumia bilionea wa nyumba za Lugumi, Dk Louis Shika kupeleka shangwe za ushindi wa mabao 5-0, Jangwani.
Yanga ilipata ushindi huo mnono dhidi ya Mbeya City mchezo wa Ligi Kuu Bara uliopigwa kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.
Katika mechi hiyo, mabao ya Yanga yalifungwa na Mzambia, Obrey Chirwa aliyepiga ‘hat trick’ huku Emmanuel Martin akifunga mawili.
Akizungumza na Championi Jumatano, Ajibu alisema katika mechi hiyo walistahili kushinda idadi kubwa ya mabao lakini matano waliyoyapata “imependeza zaidi.”
Ajibu alisema, mechi hiyo haikuwa nyepesi kama wanavyohisi mashabiki, lakini juhudi na kujituma kwa wachezaji huku wakifuata maelekezo ya kocha wao Mzambia, George Lwadamina ndizo zimewawezesha wao kupata ushindi huo.
“Nadhani haya mabao matano tuliyoyapata yamependeza zaidi, licha ya kuwa na uwezo mkubwa wa kufunga idadi kubwa ya mabao katika mechi hiyo.
“Idadi hiyo ya mabao kwa upande wangu naona imependeza, hivyo basi tujipange kwa ajili ya mechi ijayo dhidi ya Tanzania Prisons,” alisema Ajibu.
Imependeza zaidi ni msemo ambao umekuwa maarufu kwa siku za hivi karibuni baada ya kutumiwa na Dk Shika wakati akitaka kununua nyumba za mfanyabiashara Said Lugumi hivi karibuni.
Shika ameingia mkataba wa kufanya matangazo na kampuni ya kubashiri matokeo ya Sokabet.