MWANAMKE mmoja, raia wa Japan amefichua picha zinazomwonyesha alivyokonda na kubaki na uzito wa kilo 16.8 tu wakati anaokolewa kutoka katika mikono ya babu yake ambaye aliamua kumnyima chakula.
Mkazi huyo wa Kyoto, Japan, alikuwa akinyimwa chakula na babu yake katili na aliyekuwa akimpiga kila wakati tangu alipokuwa mdogo hadi alipookolewa na watu miaka kumi iliyopita kutoka katika janga hilo lililomwacha akiwa na ngozi iliyofunika mifupa na mbavu zilizochongoka.
Akisimulia mkasa huo, mwanamke huyo ambaye jina lake limefichwa, japokuwa picha zake zipo, amesema kibabu hicho kilimpiga marufuku kula bila sababu yoyote, kikawa kinamtukana na kumpiga mateke tumboni ili kumlazimisha akitapike chakula ambacho alikuwa akila kwa kujificha wakati kibabu hicho hakipo.
Katika ujumbe alioutuma kwenye mitandao ya kijamii sambamba na picha hizo, amewataka watu wanaopitia mateso kama hayo, kutafuta msaada haraka kabla mambo hayajaharibika.
Anasema aliokoka kutoka katika mkasa huo wa kutisha “zikiwa zimebaki dakika kumi tu kabla ya kufikia kifo”.
Watumiaji wa mitandao ya kijamii walipodai kwamba amefoji picha hizo, mwanamke huyo alituma picha kadhaa alizopigwa akiwa hospitali ambazo zinaonyesha majeraha kwenye kifua na shingo yake yaliyosababishwa na mateso ya kibabu hicho.
Hata hivyo, mwanamke huyo hajafichua hatua zilizochukuliwa dhidi ya babu yake huyo na kwamba watu wengine wa familia yake walikuwa wapi wakati hayo yanatendeka.
WALUSANGA NDAKI/MITANDAO/MASHIRIKA YA HABARI
Comments are closed.