The House of Favourite Newspapers

Aucho Aahidi Makombe Yanga

0

KIUNGO mkabaji mpya wa Yanga Mganda, Khalid Aucho amewaahidi mashabiki wa timu hiyo kwa kuwaambia katika msimu huu hawataacha taji lolote la ubingwa.

 

Mganda huyo alitoa kauli hiyo mara baada ya kumalizika kwa mchezo wa Kariakoo Dabi uliopigwa Jumamosi kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar ambao Yanga waliwafunga Simba bao 1-0.

 

Katika mchezo huo, Aucho alicheza namba sita huku juu yake akisaidiana na Mkongomani Yannick Bangala Litombo.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Aucho alisema kuwa, atafanya kile kilichomleta Yanga ambacho ni kuipa mataji ya ubingwa kwa kipindi chote atakachokuwa katika timu hiyo.

 

Aucho alisema kikubwa anataka kuona mashabiki wa timu hiyo wanapata furaha huku akifurahi kuwepo katika timu bora ya Yanga.

 

Aliongeza kuwa Ngao ya Jamii waliyoichukua Jumamosi ni mwanzo mzuri kwa wao kufanya vizuri katika msimu ujao ambao anaamini utakuwa wenye mafanikio.

 

“Ninafahamu mashabiki wa Yanga wana furaha kubwa ya kuona timu yao inabeba makombe katika msimu huu na kati ya hayo ni ubingwa wa ligi.

 

“Huu ni mwanzo mzuri kwetu Yanga kuendelea kuchukua makombe baada ya kuichukua Ngao ya Jamii dhidi ya wapinzani wetu Simba.

 

“Kikubwa tunahitaji ushirikiano kutoka kwa mashabiki ili kufanikisha lengo yetu ambayo ni kuchukua makombe hayo, siyo kazi rahisi lakini tutapambana,” alisema Aucho aliyeidhibiti safu ya kiungo ya Simba.

Leave A Reply